Naibu Rais wa Kenya aliyetimuliwa,
Rigathi Gachagua, amedai kuwa, " Ruto hakuwa na nia ya kufanya kazi
nami", alitaka tu kunitumia kupata watu kushinda uchaguzi", ameambia
wanahabari.
Gachagua amezungumza hayo akiwa anatoka katika Hospitali ya Karen alipokuwa anatibiwa.
Rigathi Gachagua ameendelea kudai kuwa kuna baadhi ya watu ambao wamejaribu kumuua kwa kumuwekea sumu kwenye chakula mara mbili.
"Kwa mara ya kwanza, niseme ilikuwa mnamo Agosti 30, huko Kisumu, walinzi wa siri waliingia chumbani kwangu Kisumu na kuingia kwa nguvu na mmoja wao akajaribu kunitilia sumu kwenye chakula changu, lakini tuligundua na tukaweza kuepuka mpango huo." Gachagua amesema.
"Nilitakiwa kuuawa kwa kuwekewa sumu, na mnamo Septemba huko Nyeri, timu nyingine ilikuja na kujaribu kunitilia sumu kwenye chakula ambacho kilichokusudiwa kuwa changu na Baraza la Wazee wa Kikuyu."
Rigathi Gachagua ameendelea kumshutumu Rais William Ruto na kudai kuwa amesaliti makubaliano waliokuwa nayo kabla ya kuingia madarakani mwaka 2022.
Gachagua aliongeza kuwa alilazimika kuwatimua baadhi ya maafisa wa ujasusi katika afisi yake kwa sababu hakujihisi salama.
Kulingana na Gachagua, aliyemwamini amemfanya akapitia kipindi kigumu mwaka mmoja uliopita.
"Kwa mwaka mmoja uliopita, imekuwa changamoto sana kwangu. Lakini mimi ni mtu mvumilivu sana, mvumilivu kweli. Kilichotokea Alhamisi kilikuwa kilele cha mateso na mfadhaiko ulioendelea kwa mwaka mmoja.
Gachagua aliendelea kudai kuwa tangu kulazwa katika hospitali ya Karen siku ya Alhamisi, watu walio karibu na rais ambao hawakutajwa wamekuwa wakipiga simu kubaini iwapo afya yake inazidi kuzorota.
"Ninasikia watu wake wengi
walikuwa wakipiga simu hapa (hospitalini) wakiuliza ikiwa nimekufa,
nimenusurika, kama nitapona, walikuwa wakisherehekea," Gachagua amewaambia
wanahabari wakati anatoka hospitalini.
"Ruto atawajibika iwapo
lolote litanitokea", Rigathi Gachagua amesema.