Familia ya Lucy Njeri, MCA wa kuteuliwa kutoka kaunti ya Kirinyaga, inaomboleza kifo cha binti yake, Seth Nyakio Njeri ambaye mwili wake ulipatikana katika chumba cha kukodi katika eneo la Biafra mjini Thika.
Mwanafunzi huyo wa zamani wa Chuo Kikuu cha Zetech mwenye umri wa miaka 23 anaripotiwa kuuawa na mwili wake kuachwa katika nyumba hiyo ya kukodi siku ya Jumatatu.
Inaripotiwa kwamba marehemu alikuwa amesafiri kutoka nyumbani kwao katika eneo la Kamakis hadi Thika kumtembelea rafiki yake na hata alikuwa amepost picha yake akiwa na marafiki zake Jumapili, Oktoba 20, kabla ya kuomba Ksh 1,000 kutoka kwa mamake, ambazo mwanasiasa huyo wa Kirinyaga alimtumia mara moja.
Siku ya Jumatatu asubuhi, familia ilipokea simu isiyo ya kawaida kutoka kwa rafiki wa marehemu ambaye aliwajulisha kuwa Seth ameuawa.
Familia iliarifu polisi kabla ya mwili wa msichana huyo wa miaka 23 kupatikana ukiwa uchi.
MCA huyo alisema kuwa bintiye aliondoka nyumbani kwao Kamakis Jumamosi bila tatizo lolote na alionekana mwenye furaha.
Wawili hao walizungumza hadi Jumapili lakini baada ya hapo juhudi za kumpata bintiye zikawa zimeambulia patupu; simu na meseji zake zilienda bila kujibiwa na jambo hilo lilimsumbua mzazi huyo.
Shughuli za kumtafuta zilianza bila mafanikio.
Wachunguzi sasa wanaelekeza uchunguzi wao kwa rafiki wa kiume ambaye alikasirishwa baada ya kutengana.
Inashukiwa kuwa mwanaume huyo alipata taarifa kuhusu aliko msichana huyo, akamtongoza na kuishia kumuua.
Wapelelezi wamerekodi taarifa kutoka kwa rafiki wa kike Seth alikuwa amemtembelea.
Uchunguzi wa awali ulibaini kuwa alikuwa amenyongwa.
Polisi wanasema mshambulizi alimdhulumu marehemu kimapenzi kabla ya kufanya kitendo hicho cha kinyama.