logo

NOW ON AIR

Listen in Live

“Tunawakujia!” Murkomen Atoa Onyo Kali Kwa Wanaoweka Viongozi Majenezani

Murkomen aliwalaumu wazazi na baadhi ya viongozi wa kidini wanaowakingia vifua vijana wa kueneza picha hizo za AI kwamba wamefeli kwani tabia hiyo si ya kufurahikiwa bali ya kukemewa.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Habari11 January 2025 - 13:22

Muhtasari




    WAZIRI wa usalama wa ndani, Kipchumba Murkomen ametoa onyo kali kwa vijana wanaotumia mitandao kwa njia mbaya ya kuweka picha za viongozi kwenye majeneza.


    Akizungumza katika kaunti ya Uasin Gishu alikoandamana na rais Ruto katika ziara ya kimaendeleo ya siku 3 iliyoanza Alhamisi kwenye bonde la Ufa, waziri huyo alisema kwamba yeye kama waziri wa usalama wa ndani ataangalia upya suala hilo na kuwachukulia hatua wahusika.


    Seneta huyo wa zamani wa Elgeyo Marakwet alisisitiza kwamba kuna umuhimu wa viongozi na haswa kiongozi wa taifa kuheshimiwa, akisema kwamba kuweka picha yake kwenye jeneza ni kiashiria cha kutishia maisha yake.


    Murkomen aliwalaumu wazazi na baadhi ya viongozi wa kidini wanaowakingia vifua vijana wa kueneza picha hizo za AI kwamba wamefeli kwani tabia hiyo si ya kufurahikiwa bali ya kukemewa.


    “Ukiona wale wanatengeneza picha kama wameweka mtu kwa jeneza, na wanaweka kwenye jeneza kiongozi wa taifa, mimi nataka nilize, nan ataka kuuliza swali hili kwa kila mzazi humu nchini, na haswa viongozi wa kanisa wanaotetea hii tabia mbaya, na wanasiasa wote ikiwemo wale tusiokubaliana kisiasa, ikiwa kesho mwanao anaenda shule na kukutana na mwenzake ambaye wanashiriki darasa moja amemchora kwenye jeneza, bado utatetea hiyo tabia?” Murkomen aliuliza.


    “Kwa sababu wakati picha kama hiyo inapowekwa, inatuma ujumbe wa kutishia kwamba nitakuuwa. Natuko hapa tunapigia makofi tabia ambazo zimeendelezwa kwa muda mrefu.”


    “Ningependa kukuhakikishia mheshimiwa rais, mimi mwenyewe na timu yetu kwenye wizara ya usalama wa ndani, tunaenda kuliangalia upya suala hili na kuhakikisha tunawachukulia hatua kwa sababu kama hatuwezi kufanya hivyo, hatutakuwa na nchi yenye muongozo mzuri,” Murkomen alisema.



    RADIO JAMBO FREQUENCIES

    Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


    logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved