TB Joshua afungiwa akaunti ya Youtube kwa 'kuwaponya watu wa mapenzi ya jinsia moja'

Muhtasari
  • YouTube imesimamisha akaunti ya mhubiri maarufu wa Televisheni wa Nigeria TB Joshua juu ya madai ya matamshi ya chuki
  • Mhubiri huyo alisema alikuwa akikata rufaa dhidi ya uamuzi wa YouTube
Image: BBC

YouTube imesimamisha akaunti ya mhubiri maarufu wa Televisheni wa Nigeria TB Joshua juu ya madai ya matamshi ya chuki.

Shirika moja la kutetea haki liliwasilisha lalamikoa baada ya kukagua video zisizopungua saba zikimuonesha mhubiri huyo akifanya maombi ya "kuwaponya" watu wa mapenzi ya jinsia moja

Facebook pia imeondoa moja ya machapisho ambayo yanaonesha mwanamke akipigwa kofi wakati TB Joshua akimuombea na kusema anatoa "roho ya pepo".

Mhubiri huyo alisema alikuwa akikata rufaa dhidi ya uamuzi wa YouTube.

Akaunti yake ya YouTube ilikuwa na wafuasi milioni 1.8.

TB Joshua ni mmoja wa wainjilisti wenye ushawishi mkubwa barani Afrika, na wanasiasa wakuu kutoka bara zima ni miongoni mwa wafuasi wake.

Shirika la Open Democracy lenye makao yake nchini Uingereza liliwasilisha malalamiko baada ya kukagua video saba zilizochapishwa kwenye idhaa ya YouTube ya TB Joshua Ministries kati ya 2016 na 2020, ambayo inaonysha kuwa mhubiri huyo anafanya maombi "kuponya" watu wa mapenzi ya jinsia moja.

Msemaji wa YouTube aliambia OpenDemocracy kwamba akaunti hiyo ilifungwa kwa sababu sera yake "inakataza maudhui ambayo yanadai kwamba mtu ni mgonjwa wa kiakili, anaugua, au ni duni kwa sababu ya ushirika wao katika kikundi kinacholindwa pamoja na mwelekeo wa kijinsia".

Ujumbe kwenye akaunti ya Facebook ya TB Joshua Ministries uilisema: "Tumekuwa na uhusiano mrefu na wenye mafanikio na YouTube na tunaamini uamuzi huu umefanywa kwa haraka."

Video hiyo ni ya kipindi cha maombi cha mwanamke anayeitwa Okoye, iliyopeperushwa kwanza mnamo 2018.

Ndani yake TB Joshua anampiga makofi na kumsukuma Okoye na mwanamke asiyejulikana kama mara 16 hivi na kumwambia Okoye: "Kuna roho inakusumbua imejipandikiza ndani yako. Ni roho ya mwanamke," openDemocracy inaripoti.

Video hiyo ambayo ilitazamwa zaidi ya mara milioni 1.5 kabla ya akaunti ya YouTube kuishusha, baadaye inamuonesha akishuhudia mbele ya mkutano kwamba "roho ya mwanamke" ilikuwa ikiharibu maisha yake lakini alikuwa ameponywa baada ya maombi ya muhubiri huyo.

Anatangaza kwamba alikuwa ameacha kuwa na "mapenzi" kwa wanawake na "sasa nina mapenzi kwa wanaume".

Mnamo Mei 2004 Tume ya Kitaifa ya Utangazaji ilipiga marufuku vituo vya Televisheni kuonesha vipindi vya wachungaji wakifanya miujiza kwenye runinga isipokuwa ikiwa imeidhinishwa

Kulikuwa na madai kwamba baadhi ya miujiza hiyo ilikuwa bandia na ilifanywa na waigizaji.

Vituo vya Televisheni viliondoa programu za wachungaji hao ili kuepuka leseni zao kufutwa au kupigwa faini na NBC.

Lakini wakati vifaa vya kurusha matangazo bila kulipia(Ving'amuzi) viliposhuka gharama na watu wengi Nigeria kumudu kuvinunua ,Wahubiri hao walianzisha vituo vya kuendelea kupeperusha vipindi vyao vya 'miujiza'

Wanatangaza na vifaa vya kisasa na wana vituo maalum vya watoa huduma kupitia runinga ya satelaiti barani Afrika, wakionesha shughuli za makanisa na wachungaji mfululizo . Ingawa bado vipo chini ya usimamizi wa NBC, vituo hivyo viliruhusiwa kuendelea kupeperusha matangazo hayo.