Milipuko Uganda : Kundi la IS lasema lilitekeleza mashambulizi ya kujitoa mhanga jijini Kampala

Muhtasari

•Washambuliaji watatu waliokuwa kwenye pikipiki walijilipua karibu na bunge na makao makuu ya polisi mjini humo.

•Kundi la Islamic State (IS) limesema ndilo lililohusika na shambulio hilo, Shirika la Habari la Amaq linaripoti.

Image: REUTERS

Washambuliaji wa kujitoa mhanga waliulenga mji mkuu wa Uganda Kampala, na kuua takriban watu watatu na kujeruhi wengine zaidi ya 30, polisi wamesema.

Washambuliaji watatu waliokuwa kwenye pikipiki walijilipua karibu na bunge na makao makuu ya polisi mjini humo.

Idadi ya waliofariki huenda ikaongezeka, huku milipuko hiyo ikiacha sehemu za mwili zikiwa zimezagaa barabarani.

Kundi la Islamic State (IS) limesema ndilo lililohusika na shambulio hilo, Shirika la Habari la Amaq linaripoti.

Mashambulizi yalikuja ndani ya dakika tatu za kila moja. Mabomu zaidi yamepatikana katika maeneo mengine ya jiji, maafisa walisema.

"Tishio la mabomu bado linaendelea, haswa kutoka kwa washambuliaji wa kujitoa mhanga," msemaji wa polisi Fred Enanga alisema.

"Tunaamini bado kuna wanachama zaidi wa seli hizi za kigaidi za ndani, haswa kikosi cha mabomu ya kujitoa mhanga ambacho kimeundwa na ADF."

Mshambuliaji wa nne amekamatwa na fulana ya vilipuzi kupatikana, polisi walisema.

Polisi wawili walikuwa miongoni mwa waliofariki. Wengine 33 walijeruhiwa katika milipuko hiyo, wakiwemo watano vibaya sana.

Shughuli bungeni zilisitishwa na wabunge kushauriwa kutofika katika jengo hilo kufuatia mashambulizi hayo.

Magari yaliyokuwa yameegeshwa karibu na bunge yaliteketea kwa moto, huku mlipuko karibu na kituo cha polisi ukivunja vioo.

"Sauti kubwa kama inayotoka kwa bunduki kubwa ilisikika. Ardhi ilitetemeka, masikio yangu yakakaribia kuziba," Peter Olupot, mlinzi wa benki ambaye alikuwa karibu na shambulio hilo karibu na bunge, aliambia shirika la habari la Reuters.

Image: BBC

IS ilitoa taarifa kwenye kituo chake cha Telegram, kisha kuripotiwa na Shirika lake la Habari la Amaq, ikisema kwamba wanachama wake walifanya mashambulizi hayo.

Maafisa walikuwa wamelilaumu kundi la Allied Democratic Forces (ADF), kundi la waasi ambalo liliahidi utiifu wake kwa IS mwaka 2019.

Hapo awali iliundwa nchini Uganda lakini sasa lina makao yake katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ADF inazidi kufanya mashambulizi kwa jina la IS.

Kumekuwa na milipuko kadhaa ya mabomu katika wiki za hivi karibuni. Mwezi uliopita, mhudumu wa baa mwenye umri wa miaka 20 aliuawa baada ya kifaa, kilichoachwa kwenye begi la ununuzi, kulipuliwa kwenye baa moja jijini. Siku kadhaa baadaye watu kadhaa walijeruhiwa wakati mshambuliaji wa kujitoa mhanga alipojilipua ndani ya basi karibu na Kampala.

IS ilidai kutekeleza mashambulizi yote mawili, na polisi walisema kuna uhusiano wa karibu na ADF - ikiwa ni pamoja na mshambuliaji wa basi kuwa kwenye orodha ya wanachama wa ADF wanaosakwa.

Uchambuzi wa Anne Soy

Mchanganyiko hatari wa wanamgambo wa ndani na itikadi kali za kimataifa unatishia usalama wa Uganda.

ADF imejumuishwa katika miaka ya hivi karibuni na IS - na hili ni shambulio kubwa zaidi ambalo imehusishwa nalo nchini Uganda tangu kuanzisha uhusiano.

ADF pia inajulikana kama Jimbo la Afrika ya Kati la Dola la Kiislamu. Kundi la Kiislamu nchini Msumbiji linatumia jina kama hilo- na linaendesha uasi wa kikatili huko.

Wanamgambo hao wanajua vizuri maeneo wanayohudumu na wanaweza kujificha ndani ya wakazi wa eneo hilo. IS inawapa msaada wa mbinu, inasaidia kuendesha kampeni yao ya propaganda - na imewapa dhamira mpya.

Vyombo vya kijasusi vya kanda na usalama vitalazimika kufanya kazi kwa karibu zaidi ili kukabiliana na tishio hilo, na umma utalazimika kuwa na uangalifu zaidi.