Uganda yathibitisha kifo cha mhudumu wa afya mwingine kutokana na Ebola

Bi Margaret Nabisubi, 58, ni mhudumu wa afya wa nne kufa kwa Ebola,

Muhtasari

•Timu ya matabibu walipata virusi walipotibu mgonjwa wa kwanza aliyethibitishwa, ambaye alihitaji upasuaji, na wamelazwa katika hospitali ya mkoa ya Fort Portal.

•Mwanafunzi wa udaktari Mtanzania, ambaye alikuwa sehemu ya timu hiyo, alifariki dunia mwishoni mwa juma.

Image: BBC

Wizara ya afya ya Uganda imethibitisha kifo cha mhudumu mwingine wa afya, ambaye aliaga dunia alfajiri ya Jumatano.

Bi Margaret Nabisubi, mwenye umri wa miaka 58, ni mhudumu wa afya wa nne kufa kwa Ebola, kwa mujibu na waziri wa afya Dkt Jane Ruth Aceng. Timu ya matabibu walipata virusi walipotibu mgonjwa wa kwanza aliyethibitishwa, ambaye alihitaji upasuaji, na wamelazwa katika hospitali ya mkoa ya Fort Portal.

Mwanafunzi wa udaktari Mtanzania, ambaye alikuwa sehemu ya timu hiyo, alifariki dunia mwishoni mwa juma. Kando, msaidizi wa afya katika wilaya ya Kagadi alikufa kwa virusi pia.

Kulikuwa pia na mshukiwa wa kifo cha Ebola ambaye ni mkunga katika wilaya ya Mubende, aliaga dunia kabla ya kupimwa.

Wahudumu wa afya walikuwa wameelezea wasiwasi wao juu ya kutokuwa na vifaa vya kujilinda vya kutosha katika siku za kwanza za kuzuka kwa janga hilo.

Takwimu rasmi zinaonyesha kuwa kumekuwa na kesi 43 zilizothibitishwa tangu kuzuka kwa ugonjwa huo kutangazwa wiki mbili zilizopita, na kumi kati yao wamekufa.

Maafisa wa afya walisema wamefuatilia zaidi ya watu 800 wanaoshukiwa kuwa walikutana na wale ambao wameambukizwa ugonjwa huo.