Ajali yaua 50 wakiwemo watoto 10 waliozama ziwani

Watoto wasiopungua 10 walikufa maji katika ajali ya boti.

Muhtasari

•Watoto waliokufa maji wote na waliopatikana katika ziwa walikuwa na umri wa kati ya miaka saba na 14.

•Miili 40 ilipatikana pamoja na watu watatu waliojeruhiwa, mmoja wao alifariki muda mfupi baadaye.

Image: BBC

Zaidi ya watu 50 walifariki katika ajali mbili tofauti zinazohusiana na usafiri nchini Pakistan siku ya Jumapili.

Takriban watu 41 walikufa wakati basi lilipoanguka kwenye korongo na kuwaka moto kusini-magharibi, wakati kaskazini-magharibi watoto wasiopungua 10 walikufa maji katika ajali ya boti.

Waliokufa maji wote na waliopatikana katika ziwa walikuwa na umri wa kati ya miaka saba na 14.

Katika eneo la ajali ya basi, afisa wa eneo hilo alisema miili hiyo "haijatambulika". Ajali hiyo ilitokea karibu na mji wa kusini wa Bela, katika Mkoa wa Balochistan, ilipokuwa ikisafiri kuelekea mji wa bandari wa Karachi.

Afisa wa eneo hilo Hamza Anjum ameliambia shirika la habari la AFP kwamba miili 40 ilipatikana pamoja na watu watatu waliojeruhiwa, mmoja wao alifariki muda mfupi baadaye.

Manusura wawili waliosalia walikuwa katika hali "mbaya". Inasemekana basi hilo liligonga nguzo kwenye daraja kabla ya kuporomoka kwenye korongo kubwa.

“Tutachunguza sababu za ajali hiyo,” Bw Anjum alisema, akiongeza kuwa vipimo vya DNA vitatumika kubaini utambulisho wa marehemu.

Katika tukio la ajali ya boti, ilipinduka kwenye ziwa Tanda, lililpo karibu na Kohat huko Khyber Pakhtunkhwa, karibu na mpaka na Afghanistan.

Afisa wa polisi wa eneo hilo Mir Rauf ameliambia shirika la habari la AFP kwamba pamoja na wale 10 waliofariki, watoto 11 wameokolewa, huku sita wakiwa katika hali mbaya. Wengine tisa wanaaminika kupotea.

Boti waliyokuwa wakisafiria ilikuwa imebeba abiria mara mbili zaidi ya ya uwezo wake katika safari ya mchana kutoka madrasa ya eneo hilo - shule ya Kiislamu - kabla ya kupinduka. "Operesheni ya uokoaji inaendelea," Bw Rauf alisema.