Apoteza mimba baada ya mtawa wa Katoliki kukataa kutoa ambulensi kumkimbiza hospitali

Mtawa huyo anayesimamia hospitali moja alipigiwa simu mara kadhaa kuruhusu ambulensi kuenda kumchukua mama mjamzito kujifunga lakini hakupokea.

Muhtasari

• Sheria za nchi hiyo zinasema mtu anayekataa kutoa msaada kwa mtu aliye hatarini ametenda kosa.

Mwanamke aliyekuwa anajifungua apoteza mtoto baada ya sista kukataa kutoa ambulensi kumkimbiza hospitalini.
Mwanamke aliyekuwa anajifungua apoteza mtoto baada ya sista kukataa kutoa ambulensi kumkimbiza hospitalini.
Image: Maktaba// rozali

Mtawa wa kanisa katoliki ametiwa mbaroni kwa madai ya kushindwa kutoa gari la wagonjwa kwa ajili ya kumsafirisha mama mjamzito akiwa katika hali mbaya na kusababisha kifo cha mtoto wake, vyombo vya habari nchini Rwanda vimeripoti.

Sista Vestine Twizeyimana, Mkurugenzi wa Kituo cha Afya cha Kivumu, alikamatwa Aprili 12 kwa tuhuma za kupuuza kusaidia mtu aliye hatarini.

Msemaji wa Ofisi ya Upelelezi ya Rwanda (RIB), Thierry Murangira alinukuliwa akisema kwamba Sista Twizeyimana, mtaalamu wa afya, alishindwa kutoa gari la wagonjwa kutoka kituo chake cha afya licha ya kupokea simu nyingi za kuomba msaada kutoka kwa watu mbalimbali katika kituo cha afya cha Bukanda.

“Gari la wagonjwa lilikuwa na lengo la kumsafirisha mama huyo hadi Hospitali ya Gisenyi kwa ajili ya kupata msaada, lakini kushindwa kutoa gari la wagonjwa kulisababisha kifo cha mtoto,” Murangira alisema.

Tukio hilo lilitokea Aprili 10 katika Wilaya ya Rutsiro, eneo la Nyabirasi. Kwa sasa mshukiwa anazuiliwa katika kituo cha Kivumu RIB huku dozi yake ikitayarishwa kwa ajili ya kufunguliwa mashtaka.

Murangira aliendelea kusema kuwa kutojali kumuokoa mtu aliye hatarini, na kushindwa kutoa msaada pale mtu anapokuwa na uwezo wa kufanya hivyo na wakati hakuna hatari inayohusika, ni jambo lisilokubalika kwa mtu yeyote katika nafasi ya uongozi, Jarida la The New Times la nchini humo liliripoti.

"Wafanyikazi wa huduma za afya hakika wanastahili kujinufaisha wenyewe kwa sababu ucheleweshaji wowote wa huduma unaweza kuwa na matokeo makubwa," Murangira aliongeza.

Chini ya sheria ya nchini humo, mtu yeyote anayeshindwa kusaidia au kutafuta msaada kwa mtu aliye hatarini wakati yuko katika nafasi ya kufanya hivyo, na wakati hakuna hatari inayohusika, anatenda kosa.