Washukiwa 3 waliomng'oa mtoto Sagini macho wakana mashtaka

Kaino alisema kutokana na ushahidi walioukusanya, unatosha kwa washtakiwa hao kushtakiwa kwa makosa makubwa.

Muhtasari

• Mvulana huyo alipatikana akiwa ametelekezwa kwenye shamba la mahindi na kukimbizwa hospitalini.

Washukiwa watatu wanaoshtakiwa kwa kumng'oa macho Baby Junior Sagini walifikishwa mbele ya Mahakama ya Kisii mnamo Alhamisi.

Alex Ochogo, Rael Nyakerario na Pacificah Nyakerario walikula kiapo upya baada ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) kuomba mahakama kubadilisha mashtaka kutoka kwa jaribio la mauaji hadi kusababisha majeraha mabaya kwa mtoto huyo.

Watatu hao walikana mashtaka.

Washukiwa hao walishtakiwa kwa jaribio la mauaji mnamo Januari 18 mbele ya Hakimu Mkaazi Christine Ogweno katika Mahakama ya Kisii.

Mwendesha Mashtaka Hillary Kaino aliwasilisha ombi kwa mahakama kubadilisha mashtaka hayo ili kuwa na mashtaka matatu ya kusababisha majeraha mabaya mwilini kwa mujibu wa kifungu cha 4 cha kanuni ya adhabu.

Washukiwa hao wanadaiwa kung'oa macho ya Mtoto Sagini mnamo Desemba 13, 2022 katika Kijiji cha Ikuruma, kaunti ndogo ya Marani, Kaunti ya Kisii.

Mvulana huyo alipatikana akiwa ametelekezwa kwenye shamba la mahindi na kukimbizwa hospitalini.

Kaino alisema ushahidi walioukusanya, unatosha kuwashtaki watatu hao kwa makosa makubwa.

George Morara ambaye ni wakili wa serikali alikubaliana na uamuzi wa kufanyia mabadiliko mashtaka. 

 

Hakimu Mkazi alisema kutokana na uzito wa kesi hiyo, mahakama ilimteua Moguche Violet na Kerosi Ondieki kuwawakilisha washtakiwa.