CITAM watoa tamko kufuatia mahakama kuhalalisha mikusanyiko ya LGBTQ

“Kwa sababu sisi ni Wakritsto, tunachukia dhambi hiyo lakini tunawapenda watenda dhambi kwa mapenzi ya Mungu" - CITAM.

Muhtasari

• Yeyote ambaye anasumbuliwa katika hilo amekaribishwa katika kanisa letu kwa ushauri nasaha pamoja na maombi - CITAM.

Askofu mkuu wa kanisa la CITAM, Calisto Odede.
Askofu mkuu wa kanisa la CITAM, Calisto Odede.
Image: CITAM

Kanisa la CITAM limetoa taarifa yao kwa vyombo vya habari kufuatia uamuzi wa mahakama ya upeo mwishoni mwa wiki jana kuhalalisha mikutano ya wapenzi wa jinsia moja.

Katika barua hiyo ambayo ilitiwa saini na askofu mkuu wa kanisa hilo Calisto Odede, walisikitishwa na uamuzi huo ambao waliutaja kama wenye ukanganyifu mwingi ambao bado haukufafanua Zaidi kama pia wale wanaojihushisha na visa vya ulawiti wako katika mabano hayo ya kuruhusiwa kufanya mikutano yao ya hadhara.

“Uamuzi huu ambao kwa kiasi kikubwa unakanganya umetuacha wengi wetu tukiwa tumeshangaa ikiwa pia wavunja sheria wengine kama walawiti na wanaoshiriki mapenzi na watu wa ukoo pia wana haki kama hiyo ya kujumuika,” sehemu ya taarifa hiyo ilisoma.

Uamuzi huo uliokuja siku chache baada ya kanisa la kianglikana nchini Uingereza kutangaza kuwa litapiga kura kuwezesha maaskofu wake kutoa “Baraka za mungu” kwa ndoa za wapenzi wa jinsia moja, jambo ambalo CITAM walilaani vikali na kusema kuwa jopo la majaji hao walikuwa wanajaribu kuhitilafiana na kazi ya Mungu.

“Kwa kweli tunalaani majaji ambao walitoa uamuzi kinyume na taratibu za maumbile kutoka kwa Mungu na pia kinyume na tamaduni ambazo zinakubalika na wengi. Vile vile, tunapongeza na kufurahia sehemu ya makundi ya Wakristu ambao wametoa sauti yao kupinga vikali uamuzi huu na katika masuala ya Kibibilia,” Odede alisema.

Kanisa hilo lilitoa wito kwa wale wote ambao wanatatizika na suala la LGBTQ na ambao wangependa kupata upako ili kuondokea ‘tatizo’ hilo kutosita kufika kwenye makanisa yao kwani milango i wazi kwa wote.

“Kwa sababu sisi ni Wakritsto, tunachukia dhambi hiyo lakini tunawapenda watenda dhambi kwa mapenzi ya Mungu. Yeyote ambaye anasumbuliwa katika hilo amekaribishwa katika kanisa letu kwa ushauri nasaha pamoja na maombi, kwa maana sisi tunaamini Mungu ana uwezo wa kusamehe na kurekebisha,” barua ilisoma.

Msisitizo mkuu ulikuwa pale kwa Wakenya wote na haswa wenye Imani ya Kiksritu kusimama kidete na kupinga vikali uamuzi wa mahakama ya upeo kuhalalisha mikutano ya LGBTQ.