Mwalimu aliyemchapa mwanafunzi wa miaka 9 viboko 104 ashtakiwa kwa jaribio la mauaji

Mwalimu huyo kwa jina Jackson Marucha kutoka kaunti ya Nyamira alidaiwa kumpa adhabu hiyo kali mtoto wa miaka 9 mwezi Machi mwaka jana, 2023 na kumuumiza vibaya kwenye makalio.

Muhtasari

• Upande wa mashtaka ulifichua maelezo ya kuhuzunisha kuhusu hali ya mwanafunzi huyo.

• Mahakama ilisikia kwamba mwanafunzi alipata hematoma, mrundikano hatari wa damu iliyoganda kwenye tishu zake.

Mwanafunzi auamia baada ya kuchapwa viboko 100
Mwanafunzi auamia baada ya kuchapwa viboko 100
Image: Kiss100

Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) imependekeza mwalimu aliyemchapa mwanafunzi wa miaka 9 hadi viboko 104 kufunguliwa mashtaka ya kujaribu kuua.

Mwalimu huyo kwa jina Jackson Marucha kutoka kaunti ya Nyamira alidaiwa kumpa adhabu hiyo kali mtoto wa miaka 9 mwezi Machi mwaka jana, 2023 na kumuumiza vibaya kwenye makalio.

Maafisa wa upelelezi walikuwa wamependekeza mshukiwa afunguliwe mashtaka ya kushambulia lakini baada ya kukagua zaidi, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) ilipendelea mashtaka ya kujaribu kuua.

Kupigwa kwa viboko kupita kiasi kulisababisha majeraha makubwa kwenye makalio ya mtoto, hivyo kuhitaji matibabu ya haraka.

Upande wa mashtaka ulifichua maelezo ya kuhuzunisha kuhusu hali ya mwanafunzi huyo.

Mahakama ilisikia kwamba mwanafunzi alipata hematoma, mrundikano hatari wa damu iliyoganda kwenye tishu zake.

Hali hii, kulingana na shahidi wa upande wa mashtaka, inaweza kuwa na matokeo mabaya ikiwa vifungo vya damu vingehamia kwenye viungo muhimu vya mwili.

"Ikiwa damu iliyoganda ingesafiri hadi kwenye mshipa, inaweza kuwa imetoka moyoni," shahidi huyo alithibitisha.

Inasemekana kwamba mwalimu huyo alimchapa viboko mwanafunzi huyo baada ya kuripoti kuwa sare zake za shule ziliibiwa kwenye kamba.

Mshukiwa huyo anasemekana kujaribu kuficha kitendo hicho kiovu kwa kumfungia mvulana huyo kwenye chumba cha kulala na kumnyima matibabu baada ya kufahamu jinsi majeraha yake yalivyokuwa makali.

Tukio hilo lilijiri baada ya wanafunzi wenzake kumjulisha mjomba wa mtoto huyo ambaye alikuwa amekwenda kumtembelea shuleni kuhusu tatizo lake.

Mjomba wa mvulana huyo aliripotiwa kuzuiwa kumuona na wasimamizi wa shule kabla ya kufichuliwa na wanafunzi wenzake.

Mwalimu mkuu wa shule hiyo Isabella Kumenda na wasaidizi wake wanne walihojiwa na wapelelezi.

 

Kumenda alidai kuwa alikuwa mbali na shule wakati tukio hilo likitokea.