Fahamu dawa iliyokuwa itibu tatizo la moyo 'bahati mbaya' ikageuka tiba ya nguvu za kiume

Image: BBC

Viagra ilianza kuuzwa mnamo 1998 na ilivyoingia sokoni tu ikafanya vizuri mara moja.

Iligunduliwa na kampuni ya dawa Pfizer, "kidonge cha bluu" ikazalisha pesa za kutosha. Katika miezi mitatu ya kwanza pekee, Wamarekani walitumia wastani wa dola milioni 400 kununua dawa ya kukosa nguvu za kiume.

Haikuchukua muda mrefu kwa sekta hiyo kuweka malengo yake katika nusu nyingine ya soko, upande wa wanawake, na kuona fursa ya kuongeza faida yake maradufu.

"Nilianza kusoma fiziolojia ya kijinsia wakati Viagra ilipokuja. Na hisia ilikuwa kwamba wakati huo, pesa nyingi zilianza kuingia katika utafiti wa ngono," anakumbuka Nicole Prause, mwanasayansi na mtafiti katika Chuo Kikuu cha California, Los Angeles (UCLA).

"Hatujawahi kuona chochote cha ukubwa huu. Sayansi yetu [fiziolojia ya ngono] bado imetengwa kwa kiasi fulani, inachukuliwa kuwa eneo hatari. Kuna kampuni nyingi ambazo hazitaki hata kuwa karibu na mada hii."

Lakini takriban miaka 25 na mamilioni mengine mengi ya dola yaliyofuata baadaye, tasnia ya dawa haijawahi kupata toleo la "kidonge cha bluu" kwa ajili ya wanawake.

Kushindwa huko, kumefungua nafasi kwa mjadala mpana juu ya masuala ya kujamiiana kwa upande wa wanawake, pia ni inahusisha simulizi kuhusu miiko na imani potofu kuhusu hamu ya wanawake kwenye tendo la ndoa, kama ilivyoangaziwa na wataalam.

Historia ya utafutaji wa "kidonge cha pinki"

Historia ya 'viagra' ama dawa za kuongeza nguvu za kiume inajulikana sana.

Dawa inayotumiwa leo kwa tatizo la upungufu wa nguvu za kiume iligunduliwa kwa bahati mbaya: "Tulikuwa tukitengeneza dawa ya angina, tatizo la moyo," Dkt. Mitra Boolell, ambaye alifanya kazi katika idara ya utafiti ya Pfizer nchini Uingereza, anaiambia BBC Brazil.

"Wakati huo baadhi ya washiriki wa majaribio ya kliniki walianza kuripoti kuwa nguvu za kiume zaidi kuliko kawaida. Hapo awali hatukuzingatia sana, tulifikiri ni kwa sababu washiriki walikuwa vijana."

Uamuzi wa kuchunguza zaidi ulikuja wakati makala iliyochapishwa na watafiti wa Marekani ilionyesha namna moja ya vipengele vya dawa ya kulevya waliyokuwa wakijaribu (kinachojulikana kama kizuizi cha PDE5) kilifanya kazi kwenye tishu za corpus cavernosum ya viungo vya kiume, na kuongeza mzunguko wa damu katika eneo hilo. .

"Bosi wangu aliniuliza niandae utafiti ili kujua kama hii ilikuwa kweli au 'ajali," anakumbuka Boolell.

Utafiti wa baadaye kuhusu viagra ungeonyesha kuwa mzunguko huu ulioongezeka unaweza kusababisha viungo vya uzazi kuwa imara na kudumu kwa muda mrefu

"Tishu zinazozalisha viungo vya uzazi vya mwanaume na mwanamke ni sawa katika hatua za mwanzo za ukuaji wa fetasi," anaelezea Boolell.

"Tumejifunza hili kwa miaka mingi na kwa wanawake, sio rahisi kujijua, " Prause anasema. "

Dawa za aina hii zinavyoongeza ukakasi wa kisayansi kwa wanawake

Matatizo mengi ya kijinsia ya wanawake hayahusiani na mtiririko wa damu usiotosha kwenye eneo la uke, anasema Lori Brotto, profesa katika Idara ya Uzazi na Magonjwa ya Wanawake katika Chuo Kikuu cha British Columbia nchini Kanada. Sababu za kawaida kwa wanawake ni zile za zinazohusiana na kupoteza ama kupungua kwa hamu ya wao kushiriki tendo la ndoa.

Kwa wanaume, wakati huo huo, viagra haifanyi kazi bila tamaa: "uanzishaji" wa ubongo unahitajika ili kumfanya mwanaume kuwa tayari kwa tendo. Swali kubwa, katika suala hili, ni kwamba kuna utofauti kubwa ya mchakato wa 'tamaa' hii kati ya wanaume na wanawake.

Kwa maoni ya Prause, ingawa yote haya yalikuwa wazi mapema kwa wanasayansi wengi waliohusika katika utafiti wa dawa za nguvu za kike kwa wanawake, uwezo wa mauzo ulisababisha makampuni mengi ya dawa kupuuza maonyo hayo .

"Tuliwaonya kuwa haitafanya kazi," anasisitiza.

Baadaye, kama mwanafunzi aliyehitimu katika Taasisi ya Kinsey, Prause akiwa sambamba na mshauri wake mkuu, katika miaka ya mapema ya 2000, alihusika katika mradi mmoja wa wanawake wa Viagra.

Katika mkutano wa kwanza na kikundi ambacho kingefanya utafiti, kwa mshangao alikutana na: ni wanaume tu, wengi wao wakiwa na umri wa zaidi ya miaka 50, madaktari wasio na shahada ya uzamivu, wote wasio na mafunzo ya kina katika utafiti wa kisayansi.

Prause alikuwa mwanamke pekee aliyekuwepo.

Wakati anaamini kwamba wageni "walikuwa pale kwa nia nzuri, kwamba walitaka kuwasaidia wanawake na walifikiri kweli walikuwa wanakabiliwa na kitu ambacho wangeweza kufanya."

Boolell anakubali kwamba sekta ya dawa inapaswa "kuwasikiliza zaidi wanawake'.

Mnamo 2004, wakati Pfizer ilitangaza kuwa inasimamisha mradi wake wa kutengeneza dawa kwa ajili ya wanawake, ilitoa mfululizo wa mahojiano kuelezea kwa nini.

"Hakuna muunganiko kati ya sehemu za siri za wanawake na mabadiliko katika ubongo [wakati wa mwitikio wa tendo la ndoa]," alisema wakati huo.

"Kutenganishwa huko hakupo miongoni mwa wanaume. Wanaume ni kawaida anapomuona mwanamke akiwa mtupu, anaweza kujiwa na hisia za kutamani kushiriki nae tendo la ndoa, lakini kwa wanawake, kunategema mambo kadhaa."

Baada ya kutofaulu kutokana na sababu nyingi zingine zikihusisha utofauti huo wa kimaumbile, kampuni za dawa polepole zipunguza bajeti za fedha kufadhili kwenye tafiti za aina hii na utafiti mwingi kuhusu saikolojia ya ngono zilianza kufifia.

Prause, ambaye wakati huo alikuwa katika Idara ya UC ya Saikolojia kama mshirika wa utafiti, alianza kukabiliwa na upinzani wa ndani katika taasisi hiyo kuendelea kufanya utafiti kwenye eneo hilo.