•Barabara karibu na Ikulu zimewekwa vizuizi huku polisi wakiwakagua madereva ambao wanazitumia.
•Jijini Kisumu, maduka mengi yameonekana kufungwa huku kukiwa na shughuli chache tu zinazoendelea
Kuna uwepo mkubwa wa polisi wa kupambana na ghasia kwenye njia nyingi za kuingia na kutoka katika jiji la Nairobi.
Barabara karibu na Ikulu zimewekwa vizuizi huku polisi wakiwakagua madereva ambao wanazitumia.
Maafisa hao walitumwa siku ya Jumatano usiku.
Haya yanajiri huku jiji kuu na miji mingine mikuu ikijiandaa kwa awamu nyingine ya makabiliano kati ya waandamanaji na polisi.
Polisi wametakiwa kutotumia nguvu kupita kiasi wanaposhughulikia maandamano hayo.
Hadi sasa watu wanne wameuawa, watano wamejeruhiwa na mali nyingi imeharibiwa katika maandamano mawili yaliyopita nchini.
Shule nyingi jijini zilitangaza kuwa hakutakuwa na mafunzo mnamo Machi 30 kutokana na maandamano yaliyopangwa.
Shirika la Reli la Kenya lilitangaza kuwa hakutakuwa na huduma za kusafirisha abiria kwa sababu ya maandamano.
Magari mengi ya huduma za umma yameondoka barabarani kwa hofu kwani biashara nyingi zimefungwa pia.
Jijini Kisumu, maduka mengi yameonekana kufungwa huku kukiwa na shughuli chache tu zinazoendelea Alhamisi asubuhi.
Barabara nyingi kuu za mji huo pia zilisalia na watu wachache tu siku ya Alhamisi asubuhi kabla ya maandamano yaliyopangwa.
Siku ya Jumatano, Waziri wa Mambo ya Ndani Kithure Kindiki alionya Wakenya dhidi ya kushiriki katika maandamano ya vurugu, akisema polisi watawazuia kwa "gharama yoyote."
Ilikuwa ni mara yake ya kwanza kutoa taarifa tangu wahalifu waliokodiwa kuvamia biashara za kibinafsi.
Kindiki alisema matukio hayo yanaweza kugeuza nchi kuwa machafuko.