Nikiweka Biblia chini, ninawakujia - Ruto atoa notisi kwa 'cartels' wa Miraa

Kama kuna mtu ambaye anajua cartel, ni ndugu yako ama rafiki yako, mfikishie habari mapema - Ruto.

Muhtasari

• “Msikuwe na wasiwasi na biashara ya miraa. Wale macartel wasiwatishe" - William Ruto.

Rais Ruto atoa ilani kwa cartels wa miraa huko Meru
Rais Ruto atoa ilani kwa cartels wa miraa huko Meru
Image: Facebook

Rais Mteule William Ruto Jumapili katika ibada moja ya kutoa shukrani katika kaunti ya Meru, alitoa ahadi chungu nzima pindi tu atakapomaliza kula kiapo na kuapishwa ofisini kama rais wa tano wa Jamhuri ya Kenya.

Meru, kaunti ambayi inajulikana kwa zao lake la Miraa kwa wingi wakazi wake wlikuwa na hamu ya kutaka kusikia ahadi ya rais katika kuendeleza zao hilo na kuhakikisha wakulima wanafaidika kutokana na Miraa.

Rais Ruto aliwahidi kwamab anajua fika kuna baadhi ya watu wa kati wanaowalaghai na kuwahangaisha wakulima wa Miraa kwa zao lao, jambo linalowasababishia wakulima hasara kando na kuhangaishwa kushoto kulia.

Ruto alitumia mfano wa Yesu aliyeenda kanisani kipindi kimoja kulingana na Biblia na kuwafanay watu wakifanya biashara kanisani, Yesu alichukua kiboko na kuwacharaza.

Ruto alisema kwa vile wakenya wamemchagua, ni sawa na kumpa kiboko na pindi atakapomaliza kula kiapo, atawanyorosha watu hao maarufu kama ‘cartels’ hadi kulainisha sekta ya ukuzaji wa miraa.

“Msikuwe na wasiwasi na biashara ya miraa. Wale macartel wasiwatishe. Mimi mmenipatia kiboko, hawa watu nitawanyorosha. Hao niachie, nikiweka tu Biblia Jumanne chini, ni mimi na wao,” alisema Ruto huku umati ukimshangilia katika kanisa hilo.

Rais huyo aliendelea kutema moto kwa kuwaambia watu iwapo wanamjua mtu yeyote ambaye anajihusisha na biashara ya kuhangaisha wakulima wa miraa, wafikishiwe ripoti kwamba hali itakuwa mbaya kabisa upande wao.

“Kama kuna mtu ambaye anajua cartel, ni ndugu yako ama rafiki yako, mfikishie habari mapema. Mpatie notisi, mwambie yule mtu amesema anawakujia,” Ruto alisema.