• Jaji mkuu Martha Koome alimutangaza rais Ruto kama rais wa tano kabla ya rais huyo kulishwa kiapo na msajili wa mahakama
Hatimaye mchakato wa shughuli ya uchaguzi imefikia kikomo hii leo Jumanne Septemba 13 mwaka 2022 baada ya rais mteule William Ruto kula kiapo chake katika uwanja wa kimataifa wa Kasarani mbele ya umati wa wakenya zaidi ya elfu 60 pamoja na viongozi mbali mbali kutoka mataifa mbali mbali duniani.
Jaji mkuu Martha Koome alimutangaza rais Ruto kama rais wa tano kabla ya rais huyo kulishwa kiapo na msajili wa mahakama na baadae kutia sahihi katika stakabadhi za kuonesha kwamab ndiye rais mteule wa tano.
Baadae ilikuwa ni wakati wa naibu rais mteule Rigathi Gachagua ambaye pia alisoma kiapo chake cha kuwahudumia wananchi wa Kenya katika ofisi ya naibu rais kwa miaka mitano ijayo.
Awali rais Uhuru Kenyatta alifika katika uwanja huo ili kuhakikisha makabidhiano ya amani ya uongozi kwa mrithi wake.
Kenyatta kwa mara ya mwisho alikagua gwaride la heshima lililoandaliwa na majeshi ya ulinzi katika vitengo vyote kabla ya kuelekea katika jukwaa kuu kuhudhuria hafla hiyo ya kihistoria.
Wakati jaji Koome anamtambulisha Ruto kama rais, umati haukutulia kabisa kwani wengi wa wafuasi wa Ruto na Wakenya wengi waliokuwa wakisherehekea uongozi mpya kabisa nchini walikuwa hawashikiki kabisa.
Jaji mkuu alimaliza kwa kutia sahihi katika stakabadhi hizo zote kabla ya kufungwa rasmi na kumkabidhi Gachagua na Ruto vyeti vya kuwa rais wa tano wa Kenya kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.