Ajuza,75, alilia haki baada ya mahindi yake kufyekwa na watu wasiojulikana usiku

Bi kizee huyo alipigwa na butwaa baada ya kuamka asubuhi na kupata mahindi yake yamefyekwa.

Muhtasari

• Nyanya aliachwa akikadilia hasara kubwa ya kukatwa kwa mahindi shamba la ekari kubwa.

Nyanya alilia mazao yake kufyekwa shambani
Nyanya alilia mazao yake kufyekwa shambani
Image: Karangu Muraya

Ajuza mmoja kutoka eneo la Nyahururu analilia haki baada ya kufyekwa kwa mahindi yake shambani yaliokuwa bado hayajakomaa.

Asuhuhi ya kuamkia Novemba 14 nyanya huyo alipata mahindi yake aliyopanda kwa ekari kadhaa za shamba na ambayo yalikuwa karibu kukomaa yamekatwa.

Tukio hilo lilimletea hasara na wasiwasi mwingi huku akiwaza iwapo atapata chakula cha kuvuna msimu huu na kuhofia njaa ambayo inaweza kumpata.

Kuharibiwa kwa mazao hayo kulimfanya mwinjilisti Karangu Muraya kustaajabu tukio hilo kupitia chapicho la video kwenye ukurasa wake wa Facebook.

''Tazama kitu walichofanya kwa shamba nzima ya nyanya Tabitha jana usiku.Sasa nyanya huyu mkongwe atapata haki wapi'' Muraya aliandika kwa kufadhaika.

Mbali na hayo mwimbaji huyu aliitaka idara ya polisi kuingilia kati ili kuhakikisha waliotekeleza kitendo hicho wamekamatwa na sheria kuchukua mkondo wake.

Tukio la kufyekwa kwa mahindi ya nyanya huyo limezua hisia  kwa wanamitandao wengi wakikashfu walio tekeleza kitendo hiki kwani ni la ukosefu wa utu.

Kamindo alisema. ''Utu ulienda wapi nchini mwetu?Inasikitisha kuona wengine wakikufa na njaa kunao wengine wanaharibu mazao'' 

Ciku Ciru alisema ''Hivi ni vibaya wamefanyia nyanya huyu na vyenye serikali inajitahidi kutafuta mahindi'' 

Kisa hiki kinaaminika kuhusishwa na watu wasiomtakia mema baada ya kutolewa gerezani na Karangu Muraya mnamo Oktoba 18, 2022.

Ajuza huyo anayejulikana kama Tabitha Osoro William alikuwa amefungwa katika Gereza la Wanawake la Nyahururu kutokana na mzozo wa ardhi.