Kisii: Arati kulipa KNEC kuchunguza uhalali wa vyeti vya wafanyikazi wa kaunti

"Tutatathmini vyeti vya wafanyikazi wetu zaidi ya 5900. Kwa hivyo mtaona watu wakipiga nduru,” Arati alisema.

Muhtasari

• Huu mchakato ndio mwanzo mkoko unaalika maua, lazima tung’arishe Kisii yetu, lazima tutamlika, - Arati.

Gavana wa kaunti ya Kisii
Gavana wa kaunti ya Kisii
Image: Facebook

Gavana wa Kisii Simba Arati ameemdeleza umakini wake katika kumaliza ufisadi kabisa kwenye kaunti hiyo.

Hii ni baada ya kutangaza kwamba anatathmini kushirikiana na bodi ya kitaifa ya mitihani KNEC ili kutathmini uhalali wav yeti vya wafanyikazi wote waliotuma maombi ya kuandikwa kwenye kaunti hiyo.

Katika video moja ambayo imesambazwa mitandaoni, gavana Arati alisema kuwa ni kweli na hatua hiyo inalenga kuhakikisha watu wanaopata kazi katika kaunti ni wale ambao wanastahili ili kuhakikisha kuna utendakazi mwema na uwajibikaji wa kimaadili.

“Ninajua haitakuwa rahisi lakini nimetoa pesa za kuhakikisha tunatathmini na kuhakikisha uhalali wav yeti kutoka KNEC, wataenda kutupatia gredi halali ambazo wafanyikazi wetu walipata kwa sababu tunajua wengi wa wafanyikazi wetu wa kaunti huenda wana vyeti bandia, hata baadhi yao huenda walijiuga vyuo vikuu kutumia vyeti vya kidato cha nne ambavyo ni bandia,” gavana Simba alinguruma.

Alisema kuwa wakati mchakato huo utakapong’oa nanga ndio muda wengi watasaga meno kwani hautakuwa muda kama kawaida wa kucheka na watu.

Arati alisema kuwa ni sharti kaunti iwe inaendeshwa na watu faafu kwa uwajibikaji mkubwa kwa pesa za mlipa kodi.

“Tutakuwa tunalipa pesa moja kwa moja kwa KNEC na walikubali kuwa watatufanyia kwa bei iliyopunguzwa kwa kiwango cha hadi nusu kwa sababu ni serikali ya kaunti kwa serikali, ili kutathmini vyeti vya wafanyikazi wetu zaidi ya 5900. Kwa hivyo mtaona watu wakipiga nduru,” Arati alisema.

Alisema kuwa wale ambao wamekuwa wakisema yeye alighushi vyeti ndio watakutana nao uso kwa uso kuona nani ndio nani hana vyeti halali.

“Watu lazima wavune kutoka kule ambako wamepanda. Huu mchakato ndio mwanzo mkoko unaalika maua, lazima tung’arishe Kisii yetu, lazima tutamlika,” gavana huyo alitoa tamko kali.

 Itakumbukwa miezi michache iliyopita gavana Arati aligonga vichwa vya habari baada ya kuangusha mjeledi kwa madereva waliokuwa wameandikwa na kaunti pasi na kupewa magari ya kufanyia kazi.

Katika zoezi hilo lililonuia kuwatumbua wafanyikazi hewa, Arati alisema kuwa madereva waliokuwa katika orodha rasmi ya kaunti walikuwa zaidi ya mia mbili hali ya kuwa magari ya kaunti yalikuwa takribani 80 pekee.