Matakwa mapya ya Raila kabla ya mazungumzo ya kitaifa kuanza

Raila alibainisha kuwa masuala yaliyoibuliwa na vijana lazima yashughulikiwe kama kipaumbele kabla ya kuanza kwa mazungumzo hayo.

Muhtasari

• "Ninakubali kwamba haki lazima iwe kwanza kabla ya mazungumzo yoyote," alisema katika taarifa Jumapili.

KINARA WA UPINZANI RAILA ODINGA
Image: EZEKIEL AMING'A

Kinara wa upinzani Raila Odinga amepiga breki kwa mchakato wa mazungumzo uliopangwa kutoa safu mpya ya madai kwa serikali.

Raila alibainisha kuwa masuala yaliyoibuliwa na vijana lazima yashughulikiwe kama kipaumbele kabla ya kuanza kwa mazungumzo hayo.

"Ninakubali kwamba haki lazima iwe kwanza kabla ya mazungumzo yoyote," alisema katika taarifa Jumapili.

Kulingana na kiongozi huyo wa ODM, waathiriwa wote wa dhuluma za polisi lazima walipwe fidia na kesi zote zinazohusiana na maandamano zitupiliwe mbali.

Pia anataka wale wote waliotekwa nyara au waliofungwa waachiliwe, masuala yaliyoibuliwa na wahudumu wa afya na walimu wa JSS yatatuliwe.

Raila amezidi kuitaka serikali kutupilia mbali Hazina mpya ya Bima ya Afya ya Jamii (SHIF) ili kupendelea NHIF ya zamani na kuwashtaki maafisa wote wa usalama waliofanya uhalifu wakati wa maandamano.

"Maswala haya yakishatatuliwa, tunaweza kuzingatia mazungumzo ya kitaifa, na kufanywa kwa uwazi katika eneo lisiloegemea upande wowote," alisema.

Wawakilishi wa mdahalo huo, alibainisha, wanapaswa pia kutoka katika sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja na vijana, serikali, viongozi wa dini, wataalamu wa afya, wanasheria na walimu.

Alisema masuala yatakayojadiliwa yanapaswa kugusa masuala ya utawala bora, kupanda kwa gharama za maisha, kutokomeza ukabila, kupambana na rushwa na madeni na usimamizi wa fedha.

Rais William Ruto hivi majuzi alitoa wito wa kuundwa kwa kongamano la kitaifa la sekta mbalimbali ili kusaidia kushughulikia maswala yaliyoibuliwa na vijana kufuatia maandamano ya kitaifa.

Mchakato wa mazungumzo ya siku sita ulipangwa kuanza Jumatatu wiki iliyopita.

Akiwahutubia wanahabari Alhamisi iliyopita, msemaji wa Serikali Isaac Mwaura alisema kuwa upinzani na serikali bado hawajafikia makubaliano kuhusu masuala muhimu.

"Majadiliano yanaendelea ndani ya pande zote mbili. Kama mnavyofahamu, upinzani una wafuasi wake na wanapaswa kufanya mazungumzo kwanza kama sisi tunavyofanya kwa upande wetu,” alisema.

Pia alifichua kuwa hakuna orodha ya mwisho ya watu binafsi watakaoshiriki katika kongamano hilo ambalo limetolewa.

"Pia ni muhimu kutambua kwamba si lazima tuketi na kuzungumza. Tunaweza hata kutumia teknolojia na kukubaliana kuhusu masuala yoyote. Kwa hivyo tuwe na subira,” alisema.