Chebukati amshukuru mkewe, watoto kwa kumuombea kipindi cha uchaguzi

Chebukati pia alishukuru ukoo wa familia mzima pamoja na makamishna waliosimama naye kipindi hicho.

Muhtasari

• Mwenyekiti huyo wa IEBC pia alimshukuru rais Ruto kwa kuitambua tume ya IEBC kuwa yenye iliendesha uchaguzi wa haki na kweli.

akizungumza katika Bomas of Kenya mnamo Agosti 10, 2022
Mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati akizungumza katika Bomas of Kenya mnamo Agosti 10, 2022
Image: ENOS TECHE

Mwenyekiti wa tume huru ya uchaguzi na mipaka IEBC Wafula Chebukati ameisifia familia yake kwa kusimama na yeye tisti katika kipindi cha uchaguzi mkuu licha ya mawimbi makali kuibuka katika tume hiyo.

Chebukati alimshukuru mkewe Mary na wanawe watatu kwa kusimama naye katika maombi, kitu amabcho alisema kilimpa nguvu na ujasiri wa kufanay kazi yake pasi na kuyumbishwa kwa njia yoyote ile na baadhi ya watu waliotaka atoe matokeo ya uchaguzi kwa upendeleo wao.

Kando na mkewe na wanawe, Chebukati pia aliwatambua wazazi wake na ukoo mzima wa familia kwa kusimama naye kipindi hicho kilichokuwa kigumu baada ya makamishna wanne wakiongozwa na naibu mwenyekiti Juliana Cherera kuiasi tume na kujitenga na matokeo ambayo Chebukati alikuwa anatarajiwa kutangaza.

“Pia ningependa kumshukuru kwa dhati mke wangu kipenzi Mary, watoto wangu Rachel @MissChebukati, Jonathan na Emmanuel @echebukati, wazazi wangu na familia kubwa zaidi kwa maombi ya kudumu na kusimama nami wakati wa kipindi cha uchaguzi,” Chebukati aliandika kwenye Twitter yake.

Pia aliwatambua na kuwashukuru makamishna waliosimama naye baada ya lile Sakata la Agosti 15 ka kuwataja kama wajasiri ambao nchi hii itawakumbuka milele kama waliosimamia haki licha ya majaribio mengi ya kurubuniwa.

“Shukrani za pekee kwa Makamishna Prof. Abdi Guliye & Boya Molu @moluboya, Mkurugenzi Mtendaji Hussein Marjan, timu yetu katika Kituo cha Kitaifa cha Kuhesabu kura, Wasimamizi wetu wa Uchaguzi na wafanyakazi wote wa @IEBCKenya ambao walifanya kazi bila kuchoka na kustahimili vitisho ili kufanikisha Uchaguzi wa 2022 unaoaminika,” Chebukati aliandika.

Vile vile alimshukuru rais William Ruto kwa kuitambua tume hiyo kama moja ambayo ilijiboreshea pointi katika dunia nzima kwa kuendesha uchaguzi ambao haukuvuja hata kidogo.

Jana baada ya kuapishwa kama rais wa 5, Ruto aliitambua tume ya IEBC ikiongozwa na Chebukati na kusema makamishna waliostahimili vitisho ndio mashujaa wa mchakato wa uchaguzi wa mwaka huu.

“Kwa niaba ya IEBC na mimi mwenyewe, ningependa kumshukuru H.E. Rais @WilliamsRuto kwa kutambua @IEBCKenya kwa kuinua kiwango cha uadilifu na kiwango cha utumishi wa umma nchini Kenya. Ninajisikia fahari kutoa mchango wangu katika kuimarisha demokrasia nchini Kenya. Mungu aibariki Kenya,” Chebukati alishukuru.