Polisi asherehekewa kwa kumzawidi mwanafunzi maskini slippers

Mwanafunzi huyo alionekana katika hali ya kutia huruma ambako miguuni yuko peku

Muhtasari

• Baada ya kumpa zawadi hiyo, polisi alimuombea kwa Mungu kumwezesha kutimiza ndoto zake.

afisa wa polisi amtunuku mwanafunzi zawadi ya slippers
afisa wa polisi amtunuku mwanafunzi zawadi ya slippers
Image: instagram

Wakenya wengi wamejawa na furaha kwenye mitandao ya kijamii baada ya picha kusambazwa zikimuonesha afisa wa polisi akimpa mwanafunzi maskini zawadi ya kanda mbili za miguuni, almaarufu kwa lugha ya kimombo Slippers.

Katika picha hiyo iliyopakiwa kwenye ukurasa wa Tweeter na Edward Akoko ambaye ni polisi katika kituo kimoja cha polisi katika kaunti ya Kilifi, alielezea kwamba alimpata mwanafunzi huyo na kuguswa na hali yake ya kutila huruma.

Mwanafunzi huyo kwenye picha hizo anaonekana peku na polisi anamkabidhi kanda mbili rangi nyekundu.

Afisa huyo wa polisi alisema mwanafunzi huyo George anasoma katika shule ya msingi ya Kaloleni. Alimuombea kwamba Mungu amjaalie ili atomize ndoto zake masomoni baada ya kumkabidhi zawadi hiyo.

“Nimefurahi kukutana na mwanafunzi George katika shule ya msingi ya Mnyenzeni kaunti ndogo ya Kaloleni kaunti ya Kilifi na kumnunulia zawadi ndogo. Natumai Mungu atamwezesha kutimiza ndoto zake,” afisa Edward Akoko aliandika.

Wanamtandao walimsifia polisi huyo kwa kujitoa kwa mwanafunzi huyo ambaye alikuwa anaenda peku huku wengine wakipongeza na hata kumtaka kufanya mawasiliano ili wazidishe msaada kwa mwanafunzi huyo ambaye kwa hakika hali yake ilikuwa inatia huruma sana.

“Kaka hii ni ishara nzuri sana kutoka kwako...naomba unifikie ningependa kumpa zawadi pia,” mmoja kwa jina Panoh aliandika.

Wengine walionekana kumsuta kwamba zawadi hiyo ni kidogo japo walikomeshwa vikali kwani ni vitu vidogo vidogo vya kujitolea ambavyo huleta mabadiliko makubwa.

Ama kweli, askari ni binadamu pia.