(+video) Mke wangu mama wa watoto 7 alitoroka na kuolewa na kakangu mdogo - Mwanaume alia

Mwanaume huyo alieleza kwamba kaka yake anafanya biashara ya bodaboda na alitoroka na mkewe na kumuacha na watoto 7.

Muhtasari

• Mwanaume huyo alieleza kuwa nduguye mmiliki wa pikipiki alikuwa anambeba mkewe kwenda kazini kila siku kabla ya kutoroka naye kabisa.

• Mkewe alieleza kuwa mumewe alikuwa anamnyanyasa na kusema alipata mapenzi ya kweli kwa kaka mdogo.

Hadithi ya kusikitisha ya mwanaume mmoja kwa jina Simon Murefu Muyeho ambaye mkewe waliyekuwa wamezaa naye watoto saba kabla ya kumtoroka na kuolewa na ndugu yake mdogo, imetia huruma sana mitandaoni.

Mwanaume huyo alieleza kwamba mkewe, mama wa watoto saba alimtoroka yeye pamoja na watoto na kuenda kuolewa na kakake mdogo, ambapo sasa anahisi uchungu usiomithilika.

Muyeho ni baba wa miaka 56 ambaye baada ya mkewe kumtoroka anaishi na watoto wake chini ya paa moja ambapo ndani ya nyumba yao ya msonge hawana kitanda wala godoro la kulalia.

Huwa anawatandikia watoto wake gunia sakafuni kwa ajili ya kulala huku yeye akiketi kando yao kuwatazama kwa huruma jinsi wanajilaza bila hata blanketi la kujikinga kijibaridi kikali cha usiku kinachowatafuna kwa makali.

Muyeho alieleza kwamba nduguye mdogo ambaye anamiliki pikipiki ya kufanya biashara ya bodaboda alimnyang’anya mkewe na sasa wanaishi naye huku akimwachia mzigo wa kuwalea watoto wao saba peke yake.

“Kuna ndugu yangu mdogo mwenye pikipiki aliyekuwa anamchukua kutoka kazini na kumchukua kaziniambapo nilimfungulia biashara na mwishowe akaja akamchukua,” Muyeho alieleza.

Alisema kuwa kwa mara kadhaa amejaribu kuzungumza na nduguye mdogo ili kumrudishia mkewe lakini bembeleza zake zote zimeangukia katika maskio yaliyotiwa pamba.

Mwanamke huyo pia alipata nafasi ya kuzungumza na mwanablogu huyo ambapo alieleza kuwa aliamua kuolewa na kaka wa mumewe kwa sababu alikuwa anamuonyesha mapenzi ya kweli.

“Mimi nilikuwa nafanya biashara, nilikuwa nimeolewa na mume wangu lakini alikuwa mnyanyasaji sana aliyekuwa akinipiga. Ndugu yake mdogo hana shida sana na mimi na nampenda kwa sababu ananijali,” Mwanamke huyo alieleza.

Mumewe huyo mpya ambaye ni kaka mdogo kwa mume wa kwanza alieleza kwamba alikuwa akiyaona maisha ya mwanamke huyo na kakake kuwa yalikuwa na ugumu wa kupigwa na kunyanyaswa.

Alisema kuwa kumchukua kwake na kukaa naye dhamira kuu halikuwa mapenzi bali alikuwa na lengo la kumuokoa kwa kumpa msaada lakini jinsi muda ulivyozidi kusonga, mapenzi yakaota baina yao.