"Uchaguzi uliisha!" baadhi ya wakaazi wa Kisumu wakataa wito wa Odinga kutotambua rais Ruto

Juzi katika uwanja wa Kamkunji, Odinga aliwaambia wafuasi wake kuwa hawezi kutambua serikali ya rais Ruto.

Muhtasari

• "Wengi wa Wakenya wamechoka kushiriki katika maandamano hapa na pale,” mmoja alisema.

Odinga akiwa na huzuni
Odinga akiwa na huzuni
Image: Maktaba

Baadhi ya wakaazi wa kaunti ya Kisumu ambayo ni ngome ya kisiasa ya kinara wa Azimio la Umoja One Kenya Raila Odinga wamemtaka mwanasiasa huyo kukoma kurudisha taifa katika joto la kisiasa na kukubali matokeo ya uchaguzi.

Katika video moja iliyopakiwa mitandaoni na shirika moja la habari humu nchini, wakaazi hao wengi wao wanaonekana kwenda kinyume na tamko la Odinga kusema hana utambuzi wowote kwa serikali ya rais William Ruto katika kile alisema kuwa matokeo ya uchaguzi wa mwaka jana yalihitilafiwa pakubwa.

“Nilifuatilia hotuba yake pale Kamkunji na alikuwa na madai yenye uzito wa aina yake, lakini unaweza ukasema kuwa wengi wa Wakenya wamechoka. Kwa hiyo kama kuja njia nyingine nzuri ya kuleta uwiano kuliko kuita watu kwenda kwa barabara, hiyo itakuwa sawa kwa sababu wengi wa Wakenya wamechoka kushiriki katika maandamano hapa na pale,” mmoja alisema.

Wengine ambao ni wafuasi wake sugu walimtaka kukubaliana na sheria kuwa Ruto ndiye rais na kujipanga upya pengine kwa uchaguzi mkuu ujao mwaka 2027.

“Kuhusu kuwa hatambui Ruto kama rais, mimi naona sasa hivi si muda wake bali ni muda wa kumpa Ruto nafasi afanye kazi yake. Akishafanya vibaya ndio amkosoe. Matamshi yake yale, tushatoka uchaguzi na hakuna kitu, tuache maneno mengi maisha yaendelee mbele. Tunaomba tu tukae pamoja kama ndugu na tuendelee mbele, tayari Ruto ndiye rais,” Mwingine alisema.

Mwingine alisema kuwa amechanganyikiwa na jinsi Odinga anawapeleka huku wakisema kuwa wakati rais alikuwa katika kaunti za Nyanza, alituma salamu zake kwa Ruto kupitia viongozi wa eneo hilo na pia kuwahimiza kuhudhuria mikutano yake ya kimaendeleo.

“Alituma salamu zake kwa Ruto akiwa Siaya kupitia Orengo, na sasa yeye huyo ndio anasema hamtambui huyo rais. Kitu anataka ni kushikilia Watu wa Nyanza ili kuwatumia, kila mtu anajua historia na kila mtu anajua.”