Maandamano hayatapunguza bei ya mafuta-Kiraitu amwambia Raila

"Siku hizo 14 zilipita jana usiku wa manane huku Kenya Kwanza ikiwa haijafanya lolote.

Muhtasari
  • "Bei ya mafuta haijabainishwa Kenya, tunanunua mafuta kutoka nje. Haijalishi utafanya maandamano kwa muda gani

Aliyekuwa Gavana wa Meru Kiraitu Murungi amewajibu viongozi wa Azimio kwa kutaka kuchukuliwa hatua kali kuhusu gharama ya juu ya maisha.

Mkuu huyo wa zamani wa kaunti alisema gharama ya juu ya mafuta ambayo uongozi wa Raila Odinga imetaja miongoni mwa sababu za maandamano yao ya mitaani kuwa kitu kisichoweza kudhibitiwa na serikali.

"Bei ya mafuta haijabainishwa Kenya, tunanunua mafuta kutoka nje. Haijalishi utafanya maandamano kwa muda gani, iwe miezi au miaka, Waarabu wanaouza mafuta hawajui kama kuna maandamani nchini," Kiraitu alisema.

Alikuwa akizungumza Jumapili wakati wa ibada ya kanisa huko Chuka kaunti ya Tharaka Nithi.

Raila mnamo Alhamisi alizindua kile alichokitaja kama Vuguvugu la Kutetea Demokrasia (MDD) mjini Nairobi ili kushinikiza serikali ya Kenya Kwanza kushughulikia miongoni mwa masuala mengine kupanda kwa gharama ya maisha.

Alisema hatua hiyo ya halaiki itakayoanza Machi 20 ni ujumbe kwa utawala wa Rais William Ruto, ambao alisema upo ofisini kwa njia isiyo halali,  na kwamba Wakenya wamechoshwa na ahadi za uongo.

"Utawala huu haramu uliondoa bila huruma ruzuku ya Unga, umeme, petroli, dizeli, mafuta ya taa, nauli ya basi na karo za shule. Hii imefanya maisha yawe magumu kwa takriban kila Mkenya," Raila alisema.

Wito wa kuchukuliwa kwa hatua hiyo kwa wingi ulikuja baada ya kutokamilika kwa makataa ya siku 14 kwa serikali "kuondoa sera hizi zote za kikatili" Wakenya watachukua hatua za kuleta mabadiliko, Raila alisema.

"Siku hizo 14 zilipita jana usiku wa manane huku Kenya Kwanza ikiwa haijafanya lolote. Leo, tunatimiza ahadi yetu kwa Ruto na utawala wake haramu wa Kenya Kwanza. Tunaachilia nguvu za watu kuchukua hatua na kuzindua Vuguvugu la Kutetea Demokrasia," alisema. .