Kila mfungwa kupewa chakula wakati wa kusikilizwa kwa kesi kortini - CS Kindiki

Pia kila mfungwa atapewa sare mbili, kitanda na godoro kama njia moja ya kuboresha maisha yao wanapotumikia vifungo.

Muhtasari

• Kindiki pia alisema wafungwa wataruhusiwa kuzungumza na watu wa familia yao mahakamani kinyume na ilivyo katika sheria za sasa.

CS Kindiki asema kila mfungwa atapewa chakula mahakamani.
CS Kindiki asema kila mfungwa atapewa chakula mahakamani.
Image: Facebook..Kindiki.

Waziri wa usalama wa ndani profesa Kithure Kindiki amesema kuwa kuanzisha tarehe mosi mwezi Juni, wafungwa wote watakuwa wanapwa chakula cha mchana kila wanapohudhuria vikao vya kusikilizwa kwa kesi zao.

Akizungumza na wafungwa katika gereza la Mwea, waziri Kindiki alisema kuwa yapo mapendekezo mengi ambayo alipokea kutoka kwa wafungwa na kuahidi kuyatekeleza yote katika ngazi yake kama waziri wa mambo ya ndani.

Kindiki alisema kuwa kando na wafungwa kuruhusiwa kupata chakula wakati wa kusikilizwa kwa kesi, pia wataruhusiwa kuwa na mazungumzo na ndugu wa karibu kutoka familia, jambo ambalo sasa hivi ni marufuku.

“Mmeuliza kuhusu chakula cha mchana kwa wale wanaoenda katika kusikilizwa kwa kesi na pia kuruhusiwa kuongea na familia. Mimi sioni tatizo lolote katika kuongea na watu wa familia. Kitu najua bajeti huenda haitakuwa ya kutosha kuwapa chakula lakini tutahakikisha kila afisa na mfungwa anayehudhuria kesi atapata chakula cha mchana. Kwa hiyo kuanzia Juni mosi kila mfungwa lazima atapewa chakula,” Kindiki alisema.

Waziri huyo pia alisema kuwa kila mfungwa atakabidhiwa kitanda chake mwenyewe pamoja na godoro ili kuboresha maisha yao wanapohudumia vifungo gerezani.

Wagungwa pia watapewa kila mmoja sare mbili mpya na wale wa makosa madogo madogo kupewa adhabu za nje ya jela kama njia moja ya kupunguza mrundiko wa wafungwa gerezani.