Fahamu sababu za Elon Musk kuachia ngazi kama CEO wa Twitter mwaka 1 baada ya kuinunua

Musk alinunua Twitter mwaka jana kwa dola bilioni 44 na kujitwika jukumu la Afisa Mkuu mtendaji.

Muhtasari

• Mnamo Desemba, Musk aliwauliza wafuasi wake wa Twitter ikiwa anapaswa kujiuzulu kama Mkurugenzi Mtendaji, na 57.5% walisema ndio.

Image: Reuters

Mmiliki wa Twitter, Elon Musk ametangaza kuachia ngazi kama afisa mkuu mtendaji wa mtandao huo mwaka mmoja tu baada ya kuununua kwa kimbunga, kwa Zaidi ya dola bilioni 44.

Musk kupitia ukurasa wake wa Twitter Alhamisi alitangaza kwamba ataachia ngazi hiyo na tayari ashampata CEO mpya ambaye ataanza kazi chini ya wiki 6 zijazo.

Hata hivyo, Musk hakumtaja CEO huyo mpya na yeye alisema kuwa atarejelea majukumu yake kama mwenyekiti mkuu ambaye kazi yake itakuwa kuangalia maendeleo ya mtandao huo.

“Nina furaha kutangaza kwamba nimeajiri Mkurugenzi Mtendaji mpya wa X/Twitter. Ataanza kazikatika ~ wiki 6! Jukumu langu litabadilika hadi kuwa mwenyekiti mtendaji & CTO, kusimamia bidhaa, programu na mifumo,” Musk alisema.

Jarida la Wall Street linaripoti kwamba Mtendaji mkuu wa NBC Universal Linda Yaccarino yuko kwenye mazungumzo ya kuwa afisa mkuu mtendaji wa Twitter.

Musk alinunua Twitter kwa dola bilioni 44 mwaka jana na alionyesha kuwa atasimamia kama CEO kwa muda mfupi tu kukamilisha marekebisho ya shirika ambayo alifikiria kampuni hiyo ilihitaji kufanikiwa.

Musk alilalamika kuwa na "kazi nyingi" na kulala katika makao makuu ya Twitter ya San Francisco huku akitekeleza mabadiliko makubwa.

Mnamo Desemba, Musk aliwauliza wafuasi wake wa Twitter ikiwa anapaswa kujiuzulu kama Mkurugenzi Mtendaji, na 57.5% walisema ndio.

Bilionea huyo atasalia kuwa mwenyekiti mtendaji baada ya kipindi cha mpito.

Musk, ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Tesla Inc. na Space Exploration Technologies Corp., amekosolewa kwa mabadiliko yake ya ghafla ya sera kwenye Twitter na kupuuza biashara zake zingine.