Isiolo: Mwanahabari apoteza 116K kwa wezi wa 'SIM swap' na 'SIM Upgrade'

Katika taarifa kwa polisi, mwanahabari huyo alisema alikuwa anaelekea nyumbani wakati walaghai wawili walimsimamisha na kujitolea kumboreshea laini kutoka 4G hadi 5G.

Muhtasari

• Alisema kuwa walaghai hao walikuwa kwa gari na baada ya kumpa laini mpya, ile yake ilianguka ndani ya gari lao na wakamtaka kutojali kwani alishapata laini iliyoboreshwa.

• Hakujali kwa sababu alikuwa na haraka ya kuwahi kwenye maombi.

Pesa za Kenya
Pesa za Kenya
Image: HISANI

Mwanahabari mmoja humu nchini anaendelea kupoza machungu ya kupoteza Zaidi ya shilingi laki moja kwa walaghai ambao walimhandaa kuwa wangemfanyia uboreshaji wa laini yake ya simu kutoka 4G hadi 5G bila malipo.

Kwa mujibu wa jarida la Nation, mwanahabari huyo Abraham Mamo alikuwa njiani kuelekea nyumbani katika kaunti ya Isiolo wakati wanaume wawili waliokuwa wamevalia sweta nyeusi walipomkaribia wakijifanya kuwa wahudumu kutoka kampuni moja ya mawasiliano humu nchini.

Mwanahabari huyo alieleza kuwa mmoja wa walaghai hao alijiita mhudumu wa nyanjani wa kampuni ya mawasiliano na wote walikuwa na vitambulisho vya kazi.

“Waliniambia niondoe laini yangu moja kwa simu ili niweze kuweka ile ambayo walikuwa wameniboreshea,” mwanahabari huyo anayefanya kazi na Kenya News Agency aliiambia Nation.

Saa moja baadae, mwanahabari huyo aligundua kwamba walaghai wale walikuwa wameiba laini yake ya simu na kufanya miamala ya pesa zake zote zipatazo elfu 116 lakini pia waliweza kufanya ombi la mkopo kupitia laini yake ya simu.

Hilo lilimfanya kupiga ripoti kwa polisi na kuweza kupata usaidizi wa kusimamisha huduma kwa laini yake, jambo lililompelekea kuokoa angalau elfu 7 ambazo zilikuwa zimesalia.

Alisema kuwa walaghai hao walikuwa kwa gari na baada ya kumpa laini mpya, ile yake ilianguka ndani ya gari lao na wakamtaka kutojali kwani alishapata laini iliyoboreshwa.

Mwanahabari huyo alikisia kwamba huenda walaghai hao walichungulia na kunakili PIN yake wakati alipokuwa akifungua simu yake baada ya kuweka laini mpya na hiyo PIN ndio ilikuwa yake kwenye mfumo wa miamala.