Wabunge wa UDA hawana heshima, wamegeuza bunge kama mtaa wa Sugoi - MP Masara

Muhtasari

• Ichungwah alisimama na kuanza kwa kauli ya utani mfupi kwamba Sugoi ni mtaa wa maana sana katika taifa la Kenya.

MP wa Suna West Peter Masara amewasuta wabunge wa UDA kugeuza bunge kuwa Sugoi
MP wa Suna West Peter Masara amewasuta wabunge wa UDA kugeuza bunge kuwa Sugoi
Image: Maktaba

Mbunge wa Suna ya Magharibi Peter Masara alizua minong’ono bungeni alasiri ya Alhamisi baada ya kuomba ruhusa kutoka kwa spika Moses Wetang’ula kutoa tamko lake.

Mbunge huyo ambaye ni mtetezi mkali wa sera za Azimio alisema kuwa wabunge wa mrengo wa serikali na haswa wale wa chama tawala cha UDA hawana heshima bungeni.

Kulingana na Masara, wabunge hao walikuwa wanazungumza na kupiga misele ya hapa na pale katika jumba la bunge wakati spika Wetang’ula alikuwa anaendelea kuzungumza.

Masara alisema kuwa kutembea tembea bungeni wakati spika anazungumza ni kukosa heshima, akiwatuhumu wabunge hao kuwa wamegeuza bunge kuwa mtaa wa Sugoi.

"Mheshimiwa Spika naona jambo la ajabu sana leo linatokea, lazima uheshimiwe. Wanachama wa UDA wanapita tu kana kwamba hapa ni mtaa wa Sugoi, ni vibaya sana bwana Spika," Masara ambaye alikuwa amesimama kwa hoja alisema.

Masara alisema haya wakati spika wa bunge alikuwa anawataarifa na kufafanua kuhusu upigani wa kura za mswada wa fedha 2023, mchakato ambao ulifanyika usiku wa Jumatano licha ya wabunge wengi kutokuwepo bungeni.

Baadae spika alimuonya Masala kwamba haikuwa lazima kwake kutoa hoja yake kwa kutumia lugha ambayo inalenga kuwadhihaki wabunge wenzake na kumpa nafasi kiongozi wa walio wengi Kimani Ichungwah kutoa hoja yake.

Ichungwah alisimama na kuanza kwa kauli ya utani mfupi kwamba Sugoi ni mtaa wa maana sana katika taifa la Kenya.

Itakumbukwa kwamba Sugoi ndio nyumbani kwa rais wa tano wa Kenya, William Ruto.