Wakenya sasa watakuwa wanatumia bidhaa za sabuni kwa matumizi ya kuoga na kufua ambazo zinatoka nje ya Kenya.
Hii ni baada ya serikali kupitia wizara ya viwanda na biashara kutangaza kwamba imetoa kibali kwa wafanyibiashara kuagiza sabuni zote kutoka nje ya Kenya.
Waziri Moses Kuria alisema kupitia Twitter kwamba serikali imefikia uamuzi huu kama hatua ya kuwalinda watumizi kutokana na bei za juu za bidhaa hizo ambazo hutengenezwa na kampuni za humu nchini.
Kuria alisema kuwa uamuzi wa serikali kuidhinisha uagizwaji wa sabuni kutoka nje ya Kenya unakuja kipindi ambapo baadhi ya watu wenye njama ya kufelisha mipango ya serikali ya rais Ruto wamepandisha bei ya bidhaa hizo.
“Katika juhudi zao potofu za kukatiza juhudi za serikali za kurahisisha tasnia ya mafuta ya kula, Mafia wenye kampuni za mafuta ya kula sasa wamepanda bei ya sabuni, jambo ambalo ni muhimu sana kwa bidhaa katika mnyororo wa thamani kwa takriban 45%. Ili kupunguza ubaya huu nimeidhinisha uingizaji wa sabuni kutoka nje ili kuwalinda watumiaji,” Kuria alisema.
Kauli ya waziri huyo wa biashara na viwanda inakuja wiki kadhaa ikionekana kukinzana na ile ambayo rais Ruto alisema na ambayo amekuwa akisisitiza kwamba analenga kuwapa vijana wa humu nchini ajira kwa kurahisisha ufunguaji na uanzishwaji wa kampuni za kutengeneza bidhaa zitakazotumiwa na Wakenya.
Wiki chache zilizopita Ruto alisema kuwa ifikapo mwaka 2025, serikali yake itapiga marufuku uagizwaji wa viatu kutoka nje ya Kenya na kuwa Wakenya wote watalazimika kutumia viatu ambavyo vimetengenezwa humu nchini kwa kutumia malighali ya humu nchini kama ngozi za mifugo.