logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Rachel Ruto aandaa tafrija ya dinner kusherehekea mwaka 1 wa Kenya Kwanza

“Kwa viongozi wote waliochaguliwa, turudi mashinani tuwatumikie wananchi wa Kenya.”

image
na Davis Ojiambo

Habari14 September 2023 - 06:01

Muhtasari


  • • Hafla hiyo iliandaliwa katika bustani ndogo ya uwanja wa Uhuru Nairobi na ilihudhuriwa na watu wachache.
Mama Rachel Ruto

Mama wa taifa Bi Rachel Ruto Septemba 13 aliandaa tafrija ya chakula cha jioni ili kuadhimisha na kusherehekea mwaka mmoja tangu serikali ya Rais Ruto ilipoapishwa na kuchukua hatamu za awamu ya tano.

Hafla hiyo iliandaliwa katika bustani ndogo ya uwanja wa Uhuru Nairobi na ilihudhuriwa na watu wachache.

Mama wa taifa alikiri kwamba mwaka mmoja wa uongozi wa mume wake, Rais Ruto ulikuwa na changamoto si haba lakini siku zote waliweka nguvu na uwepo wa Mungu mbele.

“Tulikusanyika usiku wa leo katika bustani ya Uhuru jijini Nairobi ili kutoa shukrani kwa baraka ambazo Bwana ametupa katika mwaka huu wa kwanza wa utawala huu. Mwaka uliopita umekuwa wa changamoto, lakini Mungu ametuangalia,” Rachel Ruto aliandika kwenye ukurasa wake wa mtandao wa X, awali ukijulikana kama Twitter.

Rachel Ruto ambaye amesherehekewa pakubwa kwa kuonesha ulokole wake hadharani na kujijengea sifa na taswira ya mtu ambaye ni muombaji sana na mchamungu aliendeleza wimbi hilo kwa kumshukuru Mungu kwa kuwavusha huku pia akimkabidhi usukani katika kipindi cha miaka minne iliyosalia kuelekea uchaguzi mkuu mwingine.

“Tunamshukuru sana Mungu Mkuu kwa yale aliyoyafanya; hakika ni ya ajabu machoni petu. Kama watu, tunachagua kuhesabiwa pamoja na ‘mkoma’ mmoja aliyerudi kwa Yesu kusema asante. ( Luka 17:15 ) Tunamshukuru Mungu!” alinukuu kifungu cha Biblia.

Aliwahimiza viongozi wote waliochaguliwa kurudi katika ngazi za chini walipo wananchi wapiga kura ili kueneza maendeleo katika njia ya kuboresha maisha ya kila Mkenya.

“Kwa viongozi wote waliochaguliwa, turudi mashinani tuwatumikie wananchi wa Kenya.”


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved