Siku ya Ijumaa, aliyekuwa gavana wa kaunti ya Nairobi Mike Sonko alifichua kuwa alitimiza ahadi yake ya kumpeleka aliyekuwa mwanahabari wa NTV Eunice Omollo mjini Mombasa kwa matibabu zaidi.
Bi Omollo ambaye anakabiliana na matatizo ya kisaikolojia amekuwa akipokea matibabu katika Hospitali ya Mathare na Mike Sonko hivi majuzi alikuwa ameahidi kumhamisha hadi kituo cha ukarabati cha Hospitali ya Wanawake ya Mombasa.
Katika taarifa yake siku ya Ijumaa, mwanasiasa huyo aliyezingirwa na drama nyingi alifichua kuwa Bi Omollo aliruhusiwa kutoka Mathare mnamo Alhamisi na uhamisho hadi Mombasa ukakamilika.
"Msongo wa mawazo ni hali mbaya kiafya ambayo mara nyingi husababishwa na hali ambazo mtu hawezi kudhibiti. Kama tulivyoahidi wakati wa kipindi cha Kipindi cha Obina, tulimsafirisha kwa ndege mwanahabari wa zamani wa NTV Eunice Omollo hadi Mombasa kwa matibabu zaidi katika Hospitali ya Wanawake ya Mombasa, ambako Conjestina Achieng pia anatibiwa," Sonko alisema kupitia Twitter.
Aliongeza, "Ili kumsaidia kupona, ninampa Eunice malazi ya siku 7 katika hoteli ya ufukweni. Ilikuwa ni faraja kumuona Conjestina akimkaribisha Eunice kwenye kituo hicho. Conje inaonekana amepona kabisa.”
Pia alishukuru kituo cha Mombasa Women Rehabilitation Centre kwa ushirikiano na usaidizi wao.
Mfanyabiashara huyo tajiri aliambatanisha taarifa yake na video ya matukio ya uhamisho wa Bi Omollo kutoka Nairobi hadi Mombasa.
Katika video hiyo, mwanahabari huyo wa zamani wa NTV alionekana kufurahishwa na hatua hiyo na kuahidi kupata nafuu baada ya matibabu.
"Asante sana. Ninashukuru sana, asante sana. Nitarejea hivi karibuni,” Bi Omollo alisema kabla ya kupanda ndege hadi Mombasa.
Bingwa wa zamani wa ndondi Conjestina Achieng’ ambaye amekuwa katika kituo hicho cha rehab kwa miezi kadhaa iliyopita pia alionekana akimkaribisha Bi Omollo kwa furaha katika kituo hicho.
“Hapa hivi tuko Mombasa Women’s, tunaendelea vizuri pamoja na dada yetu (Eunice) hapa hivi. Nimemshikilia mkono, tutakuwa tunaongea,” Conjestina alisema.
Alipokuwa akimkaribisha Bi Omollo, alimwambia, “Karibu Mombasa Women’s, natumaini utakuwa sawa. Hapa ndio tuko na kila kitu itakuwa sawa. Umekaribishwa sana.”
Masaibu ya Bi Omollo ilijulikana hivi majuzi ambapo katika video iliyosambazwa kwenye mitandao ya kijamii, alisikika akiangazia matatizo anayokabiliana nayo na kuomba usaidizi. Baadaye alipelekwa katika Hospitali ya Mathare ambako alikuwa amelazwa siku chache zilizopita.