Mwanamke pekee aliyekabiliwa na adhabu ya kifo amenyongwa Marekani

Muhtasari

 • Alidungwa sindano ya sumu katika gereza la Terre Haute, Indiana, baada ya Mahakama ya Juu Zaidi nchini Marekani kuamua kuondoa agizo la kuzuia kunyongwa katika dakika za mwisho.

Lisa Montgomery
Lisa Montgomery
Image: REUTERS

Lisa Montgomery - mfungwa pekee wa kike aliyekuwa anakabiliwa na hukumu ya kifo nchini Marekani- amenyongwa baada ya kutekeleza mauaji.

Alidungwa sindano ya sumu katika gereza la Terre Haute, Indiana, baada ya Mahakama ya Juu Zaidi nchini Marekani kuamua kuondoa agizo la kuzuia kunyongwa katika dakika za mwisho.

Kesi yake ilizua hisia kali baada ya mawakili wake kusema kwamba alikuwa na tatizo la kiakili lilitokana na kunyanyaswa akiwa mtoto mdogo.

Mwanamke huyo aliyekuwa na umri wa miaka 52- alimnyonga mama mja mzito kabla ya kumkata tumbo na kumteka mtoto wake katika eneo la Missouri mwaka 2004.

Mhasiriwa Bobbie Jo Stinnett, aliyekuwa na umri wa miaka 23 - alitokwa na damu hadi akafariki.

Montgomery ni mfungwa wa kwanza wa kike nchini Marekani kunyongwa katika kipindi cha miaka 67 iliyopita.

Kwa mujibu wa walioshuhudia, mwanamke aliyekuwa amesimama karibu na Montgomery wakati wa kuaawa kwake, alimuondolea usoni barakoa aliyokuwa amevaa na kumuuliza ikiwa ana jambo la mwisho angelitaka kusema. Montgomery alijibu "la", na hakuna kitu kingine.

Hatua ya kunyongwa kwake iliahirishwa mara mbili - kwanza kutokana na janga la Covid-19 wakati huo na jaji - hadi Mahakama ya Juu zaidi ilipotoa uamuzi wa kutekelezwa kwa hukumu hiyo mapema Jumatano.

Siku ya Jumatatu jaji mjini Indiana alisitisha ghafla kutekelezwa kwa hukumu hiyo hadi pale kesi ya kuchunguza hali yake ya kiakili ilipofanywa.

Mawakili wake wanasema alizaliwa na ugonjwa ulioathiri ubongo wake na kuongeza kuwa alikuwa mgonjwa sana..

Akiwa mtoto alidhulumiwa kingono na kimwili na baba yake huku mama akimsafirisha kimagendo, jamaa za familia yake walisema.

Alipitia kipindi kirefu cha ghasia na mateso wakati wa utoto wake , mawakili wake wanasema.

Lisa Montgomery ni nani?

Mnamo Desemba 2004, Montgomery aliendesha gari kutoka Kansas hadi nyumbani kwa Bobbie Jo Stinnett, huko Missouri, akidaiwa kununua mtoto wa mbwa, kulingana na taarifa iliotolewa na idara ya Sheria kwa vyombo vya habari.

"Mara baada ya kuingia nyumbani, Montgomery alimshambulia na kumnyonga Stinnett - ambaye alikuwa na ujauzito wa miezi nane - hadi mwathiriwa akapoteze fahamu," ilisema taarifa.

Montgomery alimkata tumbo mwasiriwa na kumtoa mtoto ambaye alimchukua katika jaribio la kudai kwamba ni wake.

Mwaka 2007, majaji walimpata Montgomery na kosa la utekaji nyara uliosababisha kifo, na kwa kauli moja kutoa hukumu ya kifo dhidi yake.

Lakini mawakili wake wamesema alipata dosari kwenye ubongo kutokana na kupigwa akiwa mtoto na anaugua ugonjwa mbaya wa akili.

Wafungwa wengine wanaotarajiwa kunyongwa

  • Cory Johnson alihukumiwa kwa mauaji ya watu saba, kuhusiana na kuhusika kwake na biashara ya dawa za kulevya huko Richmond, Virginia. Timu ya kisheria ya Johnson imesema kuwa ana shida ya kiakili, inayohusiana na unyanyasaji wa mwili na mihemko aliyopitia akiwa mtoto. kifo chake kimepangwa kutekelezwa tarehe 14 Januari.
  • Dustin John Higgs alihukumiwa baada ya kuhusika na vitendo vya k utekaji nyara na mauaji ya wasichana watatu mnamo mwaka 1996 Washington, DC. Higgs hakuua mwathiriwa wake yeyote, lakini alimwagiza mshtakiwa mwenzake Willis Haynes kufanya hivyo. Haynes amesema katika nyaraka za mahakama kwamba Higgs hakumtishia, au kumlazimisha afyatue risasi. Higgs amepangiwa kunyongwa tarehe 15 Januari.