Bobi Wine ahofia maisha yake: Wanajeshi wamezingira nyumba yake

Muhtasari

  • Bobi Wine amesema kwamba maisha yake yamekuwa yakitishiwa kufuatia uchaguzi wa Alhamisi ambapo rais Yoweri Museveni alihifadhi kiti chake.

  • Kampeni zilikabiliwa na ghasia ambapo makumi ya watu waliuawa.

  • Uwazi katika hesabu ya kura uliathiriwa na kukatwa kwa intaneti.

Wanajeshi wameonekana karibu na nyumba ya Bobi Wine
Wanajeshi wameonekana karibu na nyumba ya Bobi Wine
Image: GETTY IMAGES

Kiongozi wa upinzani nchini Uganda Bobi Wine amesema kwamba maisha yake yamekuwa yakitishiwa kufuatia uchaguzi wa Alhamisi ambapo rais Yoweri Museveni alihifadhi kiti chake na hivyobasi kushinda muhula wa sita kuliongoza taifa hilo.

Mwanamuziki huyo aliyebadilika na kuwa mwanasiasa aliambia BBC kwamba alikataa matokeo ya uchaguzi huo '' kwa madharau yaliostahili''.

Anadai kwamba kulikuwa na udanganyifu chungu nzima licha ya rais Museveni kuuita uchaguzi huo kuwa wa haki zaidi .

Kampeni zilikabiliwa na ghasia ambapo makumi ya watu waliuawa.

Bobi Wine anasema kwamba anawakilisha vijana
Bobi Wine anasema kwamba anawakilisha vijana
Image: EPA

Siku moja kabla ya uchaguzi huo kufanyika , serikali ilifunga intaneti , hatua ilioshutumiwa na wachunguzi wa uchaguzi huo.

Walisema kwamba uwazi katika hesabu ya kura uliathiriwa na kukatwa kwa intaneti.

Waziri mmoja wa serikali aliambia BBC siku ya Jumamosi kwamba jioni kwamba intaneti itarudishwa hivi karibuni

Je Bobi Wine alisemaje?

Katika mahojiano ya simu na BBC , Bobi Wine mwenye umri wa miaka 38 alisema kwamba ana wasiwasi kuhusu maisha yake na yale ya mkewe.

Anasema kwamba haruhusiwa kuondoka katika nyumba yake ambayo imezingirwa na vikosi vya usalama.

''Hakuna anayeruhusiwa kuondoka ama kuingia nyumbani kwetu. Pia waandishi wote wa kimataifa na wale wa nyumbani wamezuiwa kunitemebelea nyumbani'', alisema.

Akihutubia kile ambacho Chama chake National Unity Paryy kinapanga kufanya , aliambia BBC kwamba mipango yote ipo mezani ikiwemo kufanya maandamano ya amani, lakini pia akasisitiza kwamba hataki maandamano ya ghasia.

Mapema mgombea huyo wa upinzani alisema: 'Nitafurahi kusambaza video za wizi wote wa kura punde intaneti itakaporudishwa'.

Je Museveni alisema nini?

Matokeo hayo yanampatia Rais Museveni, mwenye umri wa miaka 76 , miaka mingine mitano kama rais tangu 1986.

Akizungumza baada ya kutangazwa mshindi alipinga madai ya wizi wa kura akiutaja uchaguzi huo kama uliokuwa wa haki zaidi katika historia ya taifa hilo.'

Wafusi wa Museveni walisherehekea barabarani mjini Kampala baada ya matokeo hayo kutangazwa
Wafusi wa Museveni walisherehekea barabarani mjini Kampala baada ya matokeo hayo kutangazwa
Image: REUTERS

Bwana Museveni pia alidai kwamba taifa jingine katika eneo hili lilituma maajenti ili kuingilia siasa za taifa hilo.

''Hatutakubali watu kuingilia siasa zetu hatutaki wageni kuingilia masuala yetu''.

''Iwapo uingiliaji wa masuala ya Afrika ungekuwa chanzo cha utajiri basi Afrika ingekuwa tajiri zaidi duniani''.

Wafuasi wa rais huyo walijitokeza barabarani mjini Kampala siku ya Jumamosi kusherehekea ushindi wake.