Watu 3 wapoteza maisha, 8 wajeruhiwa vibaya baada ya matatu kugongana na Lori Narok

Dereva wa matatu anaripotiwa kupoteza udhibiti wa gari kisha kugonga lori

Muhtasari

•Ajali hiyo ilitokea wakati matatu ya Galaxy ambayo ilikuwa inaelekea Kisii kutoka Nairobi iligongana ana kwa ana na lori.

•Watu wanane ambao walipata majeraha mabaya katika ajali hiyo walikimbizwa katika hospitali ya Longisa.

Watu 3 walifariki na 8 kujeruhiwa vibaya katika ajali iliyotokea Mulot
Watu 3 walifariki na 8 kujeruhiwa vibaya katika ajali iliyotokea Mulot
Image: HISANI

Watu watatu wamethibitishwa kufariki huku wengine nane wakiugua majeraha mabaya ya mwili kufuatia ajali mbaya ya barabarani iliyotokea katika eneo la Mulot, kaunti ya Narok Jumatano usiku.

Ajali hiyo ilitokea wakati matatu ya Galaxy ambayo ilikuwa inaelekea Kisii kutoka Nairobi iligongana ana kwa ana na lori lililokuwa likitoka upande huo mwingine.

Watatu ambao walipoteza uhai, wanaume wawili na mwanamke, walikuwa abiria kwenye matatu ya hiyo ya abiria 14.

Dereva wa matatu  anaripotiwa kupoteza udhibiti wa gari lake ambalo lilipotea njia na kugonga lori. Ajali hiyo ilitokea mwendo wa saa mbili unusu usiku.

Walioshuhudia ajali hiyo walisema baada ya matatu hiyo kugongana na loriilibingirika mara kadhaa kabla ya kusimama.

Kulingana na ripoti ya polisi, watu wanane ambao walipata majeraha mabaya katika ajali hiyo walikimbizwa katika hospitali ya Longisa, kaunti ya Narok ambapo wanaendelea kupokea matibabu maalum. Dereva wa matatu huyo anaripotiwa kuwa mmoja wa waliojeruhiwa huku akiugua jeraha mbaya kwenye mguu.

Miili ya watatu ambao walifariki ilipelekwa katika chumba cha kuhifadhi maiti cha hospitali ya Longisa County Referral.