Mwalimu auawa kwa kupigwa risasi nje ya shule, Baragoi

Polisi wametumwa kufuatilia wauaji na kubaini chanzo cha mauaji hayo

Muhtasari

• Mwalimu huyo wa fasihi ya Kiingereza alikuwa akielekea hospitalini katika mji wa Baragoi alipokutana na wavamizi waliompiga risasi tano kifuani.

Crime Scene

Mwalimu wa Shule ya Upili ya Wavulana ya Baragoi alipigwa risasi na kuuawa na majangili waliojihami mita chache kutoka lango la shule Jumatatu alasiri.

            Akithibitisha kisa hicho Naibu Kamishna wa Kaunti ya Samburu Kaskazini (DCC) Jackson Oloo alisema kuwa mwalimu huyo wa fasihi ya Kiingereza alikuwa akielekea hospitalini katika mji wa Baragoi alipokutana na wavamizi waliompiga risasi tano kifuani.

            Oloo alisema kuwa mwalimu huyo wa kiume aliomba ruhusa ya kwenda hospitalini kutoka kwa mkuu wa shule hiyo baada ya kuhisi maumivu asubuhi nzima.

            Aliongeza kuwa chanzo cha mauaji hayo hakijajulikana lakini polisi tayari wameanza uchunguzi huku wakiwasaka wahalifu waliotoroka.

"Vikosi vya usalama tayari vimetumwa kufuatilia wauaji na kubaini chanzo cha mauaji hayo," Oloo alisema.

            Shule ya upili ya Baragoi Boys mara kadhaa imegeuzwa kuwa uwanja wa vita kati ya jamii mbili hasimu zinazoishi katika eneo hilo.

            Tangu mwanzoni mwa miaka ya 2000, ufanisi wa shule hiyo umeathiriwa sana na ukosefu wa usalama wa kudumu huko Baragoi ambao pia ulishusha usajili wa wanafunzi kwa kiasi kikubwa huku wazazi wakiamua kuwaondoa watoto wao shuleni baada ya kuhofia maisha yao.