Polisi wapata jamaa ameficha gunia 6, mifuko 53 ya bangi ndani ya nyumba yake

Mshukiwa anaripotiwa kufanikiwa kutoroka kabla ya polisi kumtia mbaroni

Muhtasari

•Kulingana na taarifa ya Idara ya Huduma kwa Polisi, bangi yote iliyopatikana nyumbani kwa Sammy Boy ina thamani ya Ksh 500,000.

• Polisi tayari wameanzisha msako dhidi yake ili aweze kujibu mashtaka ya ulanguzi wa bangi yanayomkabili.

Gunia 6 na mifuko 53 ya bangi yenye thamani ya Ksh500,000 yapatikana Kiambu
Image: NPS

Mwanamume mmoja kutoka kaunti ya Kiambu anasakwa na maafisa wa polisi kwa madai ya kujihusisha na biashara ya bangi.

Mshukiwa ambaye ametambulishwa kama Samuel almaarufu Sammy Boy anasakwa baada ya gunia sita za mihadati hiyo haramu kupatika ndani ya nyumba yake katika mtaa wa Ucekeine Mundoro, eneo la Kiganjo, kaunti ya Kiambu.

Polisi waliovamia nyumba ya mshukiwa siku ya Alhamisi pia walipata bangi nyingine iliyokuwa imepakiwa kwenye mifuko 53 ya polythene.

Kulingana na taarifa ya Idara ya Huduma kwa Polisi, bangi yote iliyopatikana nyumbani kwa Sammy Boy ina thamani ya Ksh 500,000.

Mshukiwa anaripotiwa kufanikiwa kutoroka kabla ya polisi kumtia mbaroni. Polisi hata hivyo tayari wameanzisha msako dhidi yake ili aweze kujibu mashtaka ya ulanguzi wa bangi yanayomkabili.

"Huduma ya Kitaifa ya Polisi inasalia kujikita katika vita dhidi ya matumizi ya dawa za kulevya  na inahimiza umma kuunga mkono mafanikio kupitia kampeni za uhamasishaji na kutoa habari za haraka," Taarifa ya NPS ilisoma.

Biashara ya bangi imepigwa marufuku hapa nchini Kenya. Wanaopatika na hatia ya ulanguzi wa mihadarati hiyo wanaweza kuhukumiwa kifungo cha hadi miaka 50 gerezani kulingana na uzito wa kesi dhidi yao.