Watoto wawili wateketea hadi kufa Machakos

Mama yao alikuwa ameacha taa ikiwaka na kuwapeleka watoto wengine wawili shuleni.

Muhtasari

•Watoto hao wawili wenye umri wa miaka minne na miezi 20 walikuwa wamelala wakati wa moto huo ulipozuka Jumatatu asubuhi.

•Kisa hicho kilithibitishwa na kamishna msaidizi wa kaunti ya Matungulu Gerald Omoke ambaye alisema mama huyo alirudi na kupata nyumba ikiwa imeteketea kwa moto.

Mabaki ya nyumba ambayo watoto wawili waliteketezwa katika kijiji cha Mutalia huko Matungulu, Kaunti ya Machakos mnamo Jumatatu, Agosti 29, 2022.
Mabaki ya nyumba ambayo watoto wawili waliteketezwa katika kijiji cha Mutalia huko Matungulu, Kaunti ya Machakos mnamo Jumatatu, Agosti 29, 2022.
Image: GEORGE OWITI

Watoto wawili wamefariki baada ya moto kuteketeza nyumba katika eneo la Mutalia, kaunti ndogo ya Matungulu, kaunti ya Machakos.

Watoto hao wawili wenye umri wa miaka minne na miezi 20 walikuwa wamelala wakati wa moto huo ulipozuka Jumatatu asubuhi.

Tukio hilo lilitokea saa mwendo wa saa kumi na mbili unusu asubuhi baada ya taa ya Koroboi kulipuka na kuwasha moto katika nyumba yao ya mabati.

Mama yao alikuwa ameacha taa hiyo ikiwaka na kuwapeleka watoto wengine wawili shuleni.

Jirani mmoja alisimulia kwamba mwanamke huyo na familia yake walikuwa wamepewa nyumba hiyo ya kuishi huku wakilinda nyumba nyingine inayojengwa.

"Wavulana hao wawili hujifunza katika shule iliyoko mbali na nyumbani. Yeye huwapeleka shuleni kila siku kabla ya kumpeleka dada yao mdogo shuleni, chekechea," alisema jirani huyo.

Kisa hicho kilithibitishwa na kamishna msaidizi wa kaunti ya Matungulu Gerald Omoke ambaye alisema mama huyo alirudi na kupata nyumba ikiwa imeteketea kwa moto.

"Alipata majeraha miguuni alipokuwa akijaribu kuwaokoa watoto. Kwa sasa anapokea matibabu katika hospitali ya Kangundo level four," alisema afisa huyo wa serikali.

Aliwaonya wenyeji kuwa waangalifu wakati wa kushughulikia vyanzo vya joto ambavyo vinaweza kugeuka kuwa mbaya.

Miili ya wasichana hao wawili ilichukuliwa na polisi na kuhamishiwa hadi chumba cha kuhifadhia maiti cha Kangundo.

Uchunguzi wa tukio hilo umeanza.

UTAFSIRI: SAMUEL MAINA