Jengo la ghorofa sita laporomoka Kajiado

Mpita njia mmoja alijeruhiwa na kukimbizwa hospitali.

Muhtasari

•Jumba hilo linaripotiwa kuporomoka mwendo wa saa moja unusu usiku wa Jumatano na hakuna mtu yeyote aliyekuwa ndani wakati huo.

•Uchunguzi wa kubaini kilichosababisha nyumba hiyo kuporomoka tayari umeanza.

limeporomoka katika eneo la Oloolua, kaunti ya Kajiado.
Jengo la ghorofa sita limeporomoka katika eneo la Oloolua, kaunti ya Kajiado.
Image: HISANI

Siku chache tu baada ya jumba la ghorofa sita kuporomoka katika eneo la Kirigiti kaunti ya Kiambu, jumba lingine lenye ukubwa sawa ambalo lilikuwa likijengwa katika eneo la Oloolua, kaunti ya Kajiado limeporomoka.

Jumba hilo linaripotiwa kuporomoka mwendo wa saa moja unusu usiku wa Jumatano na hakuna mtu yeyote aliyekuwa ndani wakati huo.

Mtu mmoja aliyekuwa akipita wakati tukio hilo lilipotokea hata hivyo alijeruhiwa na kukimbizwa hospitalini. Kwa bahati nzuri aliweza kutibiwa na kupewa ruhusa kuenda nyumbani.

Uchunguzi wa kubaini kilichosababisha nyumba hiyo kuporomoka tayari umeanza.

Siku ya Jumatatu takriban watu watano walithibitishwa kufariki huku wengine kadhaa wakilazwa hospitalini baada ya jengo la ghorofa sita kuporomoka asubuhi katika eneo la Kirigiti, Kiambu mwendo wa asubuhi.

Juhudi za pamoja za kuwaokoa walionaswa zilifanywa na timu ya mashirika mengi ikiongozwa na Idara ya Kudhibiti Moto na Majanga ya Kaunti ya Kiambu, Vikosi vya Ulinzi vya Kenya, Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya, Huduma ya Polisi ya Kenya na watu wa kujitolea.

Pia alikuwepo gavana Kimani Wamatangi, Ann Wamuratha, Rosemary Kirika (naibu gavana), Joshua Nkanatha (kamishna wa kaunti) miongoni mwa viongozi wengine wa kaunti.

Akizungumza, Wamatangi alisema inasikitisha kwamba wanakandarasi hao walikiuka sheria za kuidhinisha kaunti.

Gavana huyo alibainisha kuwa kuendelea, serikali ya kaunti itakagua mradi wote wa ujenzi.