Chebukati afichua kwa nini matokeo ya maeneo bunge 27 hayakutangazwa

Chebukati alisema matokeo hayo hayakutangazwa kwa sababu ghasia ilizuka katika ukumbi huo.

Muhtasari

•Chebukati alisema makamishna walikuwa wamekubaliana kuwa kamishna Abdi Guliye ndiye atangaze matokeo hayo.

•Chebukati alisema matokeo hayo hayakutangazwa kwa sababu ghasia ilizuka katika ukumbi huo.

mbele ya jopo la uchaguzi linaloongozwa na aliyekuwa Jaji Aggrey Muchelule katika KICD, Nairobi mnamo Januari 24 2023.
Aliyekuwa mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati mbele ya jopo la uchaguzi linaloongozwa na aliyekuwa Jaji Aggrey Muchelule katika KICD, Nairobi mnamo Januari 24 2023.
Image: DOUGLAS OKIDDY

Aliyekuwa mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati amefichua sababu zilizofanya tume hiyo kutotangaza matokeo kutoka maeneo bunge 27 wakati wa kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi wa Agosti 9.

Akizungumza mbele ya jopo linalowachunguza makamishna wa IEBC siku ya Jumanne, Chebukati alisema makamishna walikuwa wamekubaliana kuwa kamishna Abdi Guliye atangaze matokeo hayo.

Alisema kuwa Guliye alipangiwa kutangaza matokeo kabla ya Chebukati kutoa tangazo la mwisho kuhusu matokeo ya mwisho ya urais.

Chebukati alisema matokeo hayo hayakutangazwa kwa sababu ghasia zilizuka katika ukumbi wa Bomas.

“Kulikuwa na matokeo ya maeneo bunge 27 ambayo yalikuwa hayajatangazwa na walikuwa wameafikiana kwamba Guliye atayatangaza,” alisema.

"Matokeo ya maeneo 27 hayakutangazwa kwa sababu ghasia zilizuka na hatukuweza kuendelea na zoezi hilo."

Chebukati alisema makamishna wanne wa zamani Juliana Cherera, Irene Masit, Francis Wanderi na Justus Nyang'aya waliachwa katika chumba cha mikutano kwa sababu hawakutaka kuungana nao kwa tangazo la mwisho.

“Hawakutaka kuungana nasi lakini naamini ni kutokana na mjadala tuliokuwa nao kuwa hatukuridhia matakwa yao ya kusawazisha matokeo,” alisema.