Knut yalalamikia uhaba wa walimu wa sekondari ya msingi

Katibu mkuu Collins Oyuu amesema ametembelea shule kadhaa na hakuna kinachoendelea.

Muhtasari

• Alitaka agizo kwamba kwa mtu kufuzu kufundisha JSS, ni lazima awe mwalimu aliyepata alama C+ katika mtihani wa KCSE kuangaziwa upya. 

Katibu mkuu wa Knut Collins Oyuu (katikati) akihutubia wanahabari mjini Kisumu. 2/3/2023.
Katibu mkuu wa Knut Collins Oyuu (katikati) akihutubia wanahabari mjini Kisumu. 2/3/2023.
Image: Faith Matete

Chama cha kutetea maslahi ya walimu nchini Kenya Knut kimelalamikia uhaba wa walimu katika Shule za Sekondari ya msingi (JSS). 

Knut siku ya Ijumaa ilidai kuwa kadri wanafunzi wengi wanavyoendelea kujiunga na JSS, masuala ya walimu yanapaswa kushughulikiwa mara moja. Katibu Mkuu wa Kitaifa wa KNUT Collins Oyuu alibainisha kuwa wengi wa wanafunzi walioripoti shuleni hawajafanya lolote kufikia sasa. 

"Tunapozungumza hivi sasa wanafunzi wameathirika vibaya. Nimetembelea shule kadhaa na hakuna kinachoendelea. Wiki nzima si muda mfupi katika mchakato wa kujifunza. Kwa hiyo tumepoteza saa kadhaa za kujifunza katika shule zetu", alisema. 

Akizungumza na vyombo vya habari mjini Kisumu, Oyuu alibaini kuwa Tume ya Huduma ya Walimu tayari ilikuwa imetangaza vigezo vya walimu wanaofaa kufunza katika shule za JSS. Oyuu alitoa wito kwa TSC kuangazia upya mambo yanaotakiwa kwa mwalimu kufuzu kufunza katika shule za sekondari ya msingi au JSS. 

Alitaka agizo kwamba kwa mtu kufuzu kufundisha JSS, ni lazima awe mwalimu aliyepata alama C+ katika mtihani wa KCSE kuangaziwa upya. 

Oyuu aliongeza kuwa takwa hili limewafungia nje walimu wengi wanaostahili kuwafundisha wanafunzi.  Katibu huyo mkuu pia aliitaka serikali kuharakisha usambazaji wa vitabu vya JSS shuleni akisema kwamba walimu wako tayari kuanza kujifunza. 

Asema kuwa baadhi ya shule hadi sasa hazijapokea baadhi ya vitabu vinavyosambazwa na zingine zimepata kitabu cha somo la Kilimo pekee.