logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Kenya yakaribia kumaliza ulipaji wa awamu ya kwanza ya Eurobond - Ruto

"Lazima tukubali kwamba kama nchi tumekuwa tukiishi maisha ghali kupita uwezo wetu."

image
na Davis Ojiambo

Habari09 November 2023 - 15:02

Muhtasari


  • • Ruto alisema kuwa baada ya kushika wadhifa wa urais, utawala wake ulilazimika kufanya maamuzi magumu ya kiuchumi ili kudhibiti hali ya uchumi wa taifa.
Rais William Ruto akitoa hotuba yake kwa taifa mnamo Novemba 9, 2023. Picha: BUNGE LA KITAIFA

Rais William Ruto ametangaza kuwa Kenya mnamo Desemba mwaka huu itakuwa imekamilisha ulipaji wa awamu ya kwanza ya Eurobond ya Dola bilioni mbili (Ksh.304B), ambayo ni kiasi cha Dola za Kimarekani milioni 300 (Ksh.45.6 bilioni).

 

Akitoa Hotuba yake katika bunge Rais William Ruto alisema kuwa baada ya kushika wadhifa wa urais, utawala wake ulilazimika kufanya maamuzi magumu ya kiuchumi ili kudhibiti hali ya uchumi wa taifa ambayo ilikuwa imedorora. Juhudi hizi, alisema, hatimaye zimeanza kuzaa matunda.

 

"Tumejitahidi sana ndani na nje ya nchi kushauriana na washirika wetu wa maendeleo ili kukomboa nchi yetu kutoka kwenye lindi la dhiki ya madeni na kutuweka leo kwenye njia thabiti ya ukuaji wa uchumi endelevu," alisema rais.

Rais aliongeza kuwa kutokana na juhudi thabiti na endelevu za Kenya kulipia deni lake la umma linalozidi kushamiri, uhusiano wa Nairobi na mashirika ya kimataifa ya kutoa mikopo kama vile Shirika la Fedha la Kimataifa, Benki ya Dunia na Benki ya Maendeleo ya Afrika umeimarika.

 

"Lazima tukubali kwamba kama nchi tumekuwa tukiishi maisha ghali kupita uwezo wetu. Wakati umefika wa kuacha starehe za uwongo na matumizi mabaya na ruzuku isiyo na manufaa kwenye matumizi na kujichimbia ndani ya shimo la madeni ambayo tungeepuka," Ruto alisema.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved