"Ningekuwa nasimamia muda, usingesafiri Joe!" Kareh B adai haki kufuatia kifo cha mwanawe

"Taa zimezimika mapema sana kwako kijana wangu," Kareh B aliomboleza.

Muhtasari

•Kareh B amendelea kuelezea uchungu wake kama mama aliyefiwa na mwanawe na amejitosa katika kudai majibu juu ya kile kilichotokea

•Familia na watu wa karibu waliweka shada la maua katika makutano ya Mamboleo, ambapo ajali iliyogharimu maisha ya Joseph ilitokea.

Mwanamuziki Kareh B na marehemu mwanawe katika picha ya kumbukumbu
Image: FACEBOOK// KAREH B

Mwimbaji mashuhuri wa Mugithi Mary Wangari Gioche almaarufu Kareh B ameendelea kuomboleza kwa uchungu kufuatia kifo cha mwanawe wa miaka 17, Joseph Mwaduli.

Joseph ambaye alikuwa mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Upili ya Wavulana ya Chavakali katika eneo la Magharibi alifariki Jumatatu usiku baada ya basi la Easy Coach walilokuwa wamepanda kuwapeleka nyumbani kwa likizo ya Aprili kuanguka katika makutano ya Mamboleo, kaunti ya Kisumu.

Kareh B amendelea kuelezea uchungu wake kama mama aliyefiwa na mwanawe na amejitosa katika kudai majibu juu ya kile kilichotokea.

“Nahitaji majibu. Laiti ningekuwa nasimamia muda, usingesafiri Joe! Lakini sina uwezo,” msanii huyo alisema katika moja ya machapisho yake kwenye Facebook.

Alishiriki picha na video zinazoangazia matukio mazuri waliyokuwa nayo na kijana huyo kabla ya kifo chake kisichotarajiwa mnamo Aprili 1, 2024.

"Taa zimezimika mapema sana kwako kijana wangu," alisema.

Siku ya Ijumaa, familia na watu wa karibu waliweka shada la maua katika makutano ya Mamboleo, ambapo ajali iliyogharimu maisha ya Joseph ilitokea.

Kareh B alikuwa ametoa tangazo kuhusu tukio hilo mapema siku hiyo, huku pia akiishukuru familia yake kwa kumjulia hali tangu ampoteze mwanawe.

"Saa kumi na mbili jioni tutaweka shada la maua katika Mamboleo ambapo ajali ilitokea.. Yeyote aliye karibu na Kisumu tafadhali jiunge nasi😭😭," Kareh B alitangaza kwenye Facebook.

Aliongeza, “Wale wanaouliza kuhusu mikutano, inaendelea Blue springs kuanzia saa kumi na mbili unusu jioni..  Asante Familia kwa kunijulia hali hadi hapa. Nenda vizuri mwanangu 😭.”

Hapo awali, mwanamuziki huyo alidai majibu kuhusu kifo cha mwanawe, akifichua kuwa hayuko sawa kufuatia tukio hilo la kusikitisha.

"Nahitaji majibu, navunjika," Kareh B alisema kupitia Facebook.

Alidai kuwa bado hajapata taarifa kuhusu kifo cha mtoto wake na kile kilichotokea. Pia alilalamikia suala la watoto wa shule kusafiri usiku.

Msanii huyo kutoka kaunti ya Murang’a pia aliitaka serikali kutoa majibu kuhusiana na ajali za barabarani, suala ambalo amewataka kushughulikia kwa dharura.

“Serikali; mna maoni gani katika Suala hili? Je, mtaendelea kuwa kimya na kupoteza watoto wengi zaidi barabarani?

Je, ni hatua gani unaweka ili kupunguza ajali zinazotokea nchini hasa vijana wa kizazi kipya? Je, tunahitaji kumfufua Michuki?” Aliandika.

Aliongeza, “Nahitaji Majibu. Nenda sawa mwanangu."