Raila ajitenga na uteuzi wa viongozi wa ODM kwa baraza la mawaziri

"Nimezingatia tangazo la Rais William Ruto jana kuhusu kuundwa upya kwa baraza la mawaziri kujumuisha wanachama wanne kutoka ODM.

Muhtasari
  • Aliongeza kuwa uteuzi huo si sehemu ya makubaliano yoyote kati ya Ruto, chama chake au Azimio la Umoja.
KINARA WA UPINZANI RAILA ODINGA
Image: EZEKIEL AMING'A

Kinara wa ODM Raila Odinga amejitenga na uamuzi wa kuwateua baadhi ya viongozi wa chama chake katika baraza la mawaziri.

Raila alishikilia kuwa chama cha ODM hakijaingia mkataba wa muungano na Rais William Ruto.

Katika taarifa yake, alibainisha kuwa Ruto aliteua wanachama wanne wa chama chake.

Aliongeza kuwa uteuzi huo si sehemu ya makubaliano yoyote kati ya Ruto, chama chake au Azimio la Umoja.

"Nimezingatia tangazo la Rais William Ruto jana kuhusu kuundwa upya kwa baraza la mawaziri kujumuisha wanachama wanne kutoka ODM.

Kama ilivyobainishwa katika taarifa yetu ya Jumanne, Julai 23, 2024, si Chama cha ODM wala Azimio la Umoja One Kenya ambacho kimeingia katika makubaliano yoyote ya muungano na chama cha UDA cha Rais Ruto.

Tulitarajia uundaji wa masharti ya wazi ya ushiriki kulingana na maswala tuliyoibua katika jumbe zetu mbalimbali,"Raila alisema.

Raila aliwapongeza wote walioteuliwa katika nyadhifa zao mpya.

"Ingawa tunawatakia kila la kheri walioteuliwa na kuamini kwamba watachangia vyema katika maendeleo ya taifa, tunaendelea kutetea mashirikiano ya kitaifa chini ya masharti tuliyotaja hapo awali kama hapa chini:

1. Fidia kwa familia za wahasiriwa wa kunyongwa nje ya mahakama na watu waliojeruhiwa na serikali tangu mwaka jana.

2. Kuachiliwa kwa watu wote walio chini ya ulinzi na kusitishwa kwa kesi zote zinazohusiana na maandamano tangu mwaka jana.

3. Mashtaka ya polisi waliohusika katika kuwapiga risasi au kuwatia ulemavu waandamanaji. ODM inasalia imara katika kushikilia kanuni zake za msingi za demokrasia, utawala bora na haki ya kijamii.

Kanuni hizi wakati wote zitaongoza matendo na maamuzi yetu tunapojitahidi kuboresha taifa letu. Tunawahimiza washikadau wote kusalia kujitolea kwa maadili ya umoja na maendeleo kwa ustawi wa Wakenya wote."