Watu 10 wajeruhiwa katika makabiliano kanisani Kisii

Makundi hayo yalikinzana katika mzozo kuhusu uongozi wa kanisa hilo.

Muhtasari

•Wanawake wawili waliovaa vilemba kichwani walionekana kutoka makundi yanayokinzana wakibishana kwa sauti kubwa ndani ya kanisa

•Hali hiyo ilizidi kuchacha mno ambapo wanachama wa makundi mawili wanapigana kwa kutumia viti vya plastiki kama silaha.

Zaidi ya watu kumi wanaugaza majeraha hospitalini baada ya kujeruhiwa kwa namna mbalimbali katika mtafaruku ulioibuka katika Kanisa la Nyabigena Adventist lililoko South Mugirango, Kaunti ya Kisii.

Mvutano huo ulikuwa baina ya makundi mawili yanayokinzana katika mzozo kuhusu uongozi wa kanisa hilo.

Katika video zinazoenea mitandaoni, inaonyesha wanawake wawili waliovaa vilemba kichwani wakionekana kutoka makundi yanayokinzana wakibishana kwa sauti kubwa ndani ya kanisa.

Ripoti zinaeleza kuwa makundi haya yanajumuisha wanachama kutoka Kanisa la Adventist na Nairobi Cosmopolitan Conference (NCC), ambayo inaripotiwa kugawanyika kutoka katika nyumba ya ibada ya Adventist.

Licha ya kutokea kwa mgawanyiko, vikundi vyote vinaendelea kufanya ibada katika eneo hilo hilo siku za Jumamosi.

Mzozo kati ya wanawake hawa unavutia umakini wa wanaume kadhaa wanaozunguka mmoja wa wanawake hao kwa nia ya kumfukuza kwa nguvu kutoka kanisani.

Mwanamke huyo anakataa kufukuzwa na anakumbana na kipigo kutoka kwa mwanamke mwingine.

Hali hiyo ilizidi kuchacha mno ambapo wanachama wa makundi mawili wanapigana kwa kutumia viti vya plastiki kama silaha.

Mtafaruku huo unaendelea kwa dakika kadhaa kabla ya kuhamia kwenye uwanja wa kanisa.

“Mpango huu umeanzishwa na baba yangu. Kundi jingine halikupaswa kuja hapa. Vibaraka walitumwa hapa kutufukuza na walitutembelea kwa njia ya kipekee kwa kutupiga kwenye harakati,” alisema Penwel Nyambane, mwanachama wa NCC aliyekuwa sehemu ya machafuko, akiiambia Citizen.

“NCC si sehemu ya Kanisa la Adventist lakini wamekuwa wakitumia ardhi yetu kwa miaka mingi,” alisema Martha Bosibori, mshiriki mwingine wa tukio hilo.

Makundi haya mawili yameapa kurudi kwenye suala hilo Jumamosi hii licha ya viongozi wao kuamriwa kufika mbele ya naibu kamishna wa Kaunti wa eneo hilo ili kutatua mzozo huo.

Wakazi wa eneo hilo wamehimiza serikali kuingilia kati na kushughulikia hali hiyo.