Martha Karua azungumza baada ya kupendekezwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali

Kiongozi wa Narc Kenya Martha Karua amefutilia mbali uwezekano wowote wa yeye kujiunga na serikali ya Kenya Kwanza.

Muhtasari

•Karua alipendekezwa kwa nafasi iliyoachwa wazi ya Mwanasheria Mkuu ikisemekana kwamba ushauri wake unafaa sana katika serikali ya rais William Ruto.

•Katika majibu yake, waziri huyo wa zamani wa sheria aliweka wazi kuwa hana nia ya kuchukua nafasi hiyo.

Martha Karua
Image: HISANI

Kiongozi wa chama cha Narc Kenya na ambaye alikuwa mgombea mwenza wa muungano wa Azimio La Umoja-One Kenya katika uchaguzi wa 2022, Martha Karua, amefutilia mbali uwezekano wowote wa yeye kujiunga na serikali ya Kenya Kwanza.

Siku ya Jumamosi asubuhi, mtumiaji wa mtandao wa Twitter aliandika posti ya kumuidhinisha mbunge huyo wa zamani wa Gichugu kwa nafasi iliyoachwa wazi ya Mwanasheria Mkuu akibainisha kwamba ushauri wake ungefaa sana katika serikali ya rais William Ruto.

Namuunga mkono @MarthaKarua kwa nafasi ya Mwanasheria Mkuu. Ushauri wake unahitajika sana na serikali. Martha anafaa kuchukua nafasi hiyo mara moja,” @PeterKariukiKE aliandika na kuambatanisha taarifa yake na bango la wasifu wa Bi Karua.

Katika majibu yake, waziri huyo wa zamani wa sheria aliweka wazi kuwa hana nia ya kuchukua nafasi hiyo.

“Asante, sitaki,” Martha Karua alijibu.

Jibu lake linathibitisha uamuzi wake mkali wa kutofanya kazi na serikali ya Kenya Kwanza.

Mnamo Alhamisi, mbunge huyo wa zamani wa Gichugu aliarifu kuhusu uamuzi wa chama chake kujiondoa katika muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya. Hii ilikuwa baada ya baadhi ya wanachama wa ODM, chama kingine kinachounda Azimio, kuteuliwa kuchukua nyadhifa za uwaziri.

Uamuzi huo uliwasilishwa katika barua iliyotumwa kwa katibu mkuu wa muungano huo, Junet Mohammed, na kaimu katibu mkuu wa Narc Kenya Asha Bashir.

"Tafadhali fahamu kuwa kukaa kwetu katika Muungano wa Azimio la Umoja One Kenya hakuwezi kudumu kutokana na maendeleo ya kisiasa yaliyopo," Bashir alisema.

“Kama NARC Kenya kwa njia ya barua hii, tunatoa notisi ya kujiondoa kwenye Muungano kama ilivyoainishwa katika kifungu cha (ma) kutoka katika Makubaliano ya Muungano. Notisi hii inaanza kutumika kuanzia tarehe ya barua hii," aliongeza.

Karua kupitia tweet alisema "Kukaa kwetu Azimio La Umoja One Kenya Alliance hakuwezi tena".

Nia ya chama chake kujiondoa Azimio ni ya mshangao ikizingatiwa hakikisho lake wakati wa mahojiano ya redio Jumanne kwamba uhusiano wake na mkuu wa muungano huo Raila Odinga ulikuwa thabiti.

"Tulizungumza muda si mrefu uliopita, na tutaweza kuzungumza tena, mambo yako wazi," Karua alisema.

Katika kukataa kuwa sehemu ya serikali ya umoja wa kitaifa, Karua badala yake alitoa wito wa kuimarishwa kwa upinzani kuendelea kuzidisha shinikizo kwa serikali ya Kenya Kwanza kutimiza ahadi zake.