Christian Atsu aokolewa akiwa hai kutoka kwa vifusi vya jengo lililoporomoka Uturuki

Wanasoka wengine, akiwemo Onur Ergun na Burak Oksuz, waliokolewa kufuatia tukio hilo.

Muhtasari

•"Christian Atsu aliondolewa kwenye mabaki na majeraha. Kwa bahati mbaya, mkurugenzi wetu wa michezo Taner Savut bado yuko chini ya vifusi," Meneja Mustafa Özat alisema.

•Wanasoka wengine, akiwemo Onur Ergun na Burak Oksuz, waliokolewa kufuatia tukio hilo.

Mchezaji wa zamani wa Chelsea Christian Atsu
Image: HISANI

Kuna habari njema kuhusu mshambuliaji wa zamani wa Chelsea na Newcastle Christian Atsu aliyekuwa amenaswa kwenye  vifusi vya jengo lililoporomoka katika mji mkuu wa Uturuki, Hatay.

Atsu ambaye kwa sasa anachezea Klabu ya Uturuki, Hatayspor alikuwa ameripotiwa kukwama kwa saa kadhaa baada ya jengo alimokuwa na baadhi ya wachezaji wenzake kuporomoka usiku wa kuamkia Jumatatu.

Taarifa kutoka Uturuki sasa zinaarifu kwamba raia huyo wa Ghana mwenye umri wa miaka 31 ameweza kuokolewa akiwa hai siku ya Jumanne asubuhi na kukimbizwa hospitalini kwa matibabu maalum.

"Christian Atsu ametolewa kwenye mabaki akiwa hai!" mtangazaji wa Uturuki  Yagiz Sabuncuoglu alitangaza.

Meneja wa klabu ya Hatayspor Mustafa Özat alisema, "Christian Atsu aliondolewa kwenye mabaki na majeraha. Kwa bahati mbaya, mkurugenzi wetu wa michezo Taner Savut bado yuko chini ya vifusi."

Hatayspor, klabu ya sasa ya Atsu, iko katika jiji la Uturuki la Hatay, ambalo linaaminika kuwa moja ya maeneo yaliyoathiriwa zaidi na tetemeko hilo la ardhi lenye ukubwa wa 7.7 kwenye richa lililotokea Jumatatu.

Wachezaji wengine, akiwemo Onur Ergun na Burak Oksuz, waliokolewa kufuatia tukio hilo. Wenzake Atsu wawili, Ruben Ribeiro na Ze Luis, wako salama, huku Kerim Alici akifanikiwa kujinasua kutoka kwenye vifusi.

Atsu, 31, alijiunga na klabu ya Super Liga, Hatayspor kutoka akitokea Al-Raed ya Saudia msimu uliopita.

Hapo awali aliwahi kuchezea Chelsea, Newcastle, Everton na Bournemouth katika ligi kuu ya Uingereza, EPL.