Wajackoyah amteua naibu mpya wa chama huku kukiwa na mzozo kati yake na Wamae

Chama cha Roots kimemteua Vinod Ramji kama Naibu Kiongozi wa Chama.

Muhtasari

•Wajackoyah na mgombea mwenza wake Justina Wamae walitofautiana kwa madai kuwa Wamae  anawakilisha vibaya msimamo wa chama.

•Wamae aliitwa Ijumaa na chama kufuatia matamshi yake.

Mgombea urais Wajackoyah,wakati wa mahojiano na Radiojambo 10/juni/2022
Image: CHARLENE MALWA

Chama cha Roots kimemteua Vinod Ramji kama Naibu Kiongozi wa Chama.

Haya yanajiri siku chache baada ya kiongozi wa chama George Wajackoyah na mgombea mwenza Justina Wamae kutofautiana kwa madai kuwa anawakilisha vibaya msimamo wa chama.

Katika tangazo, chama hicho pia kilimteua Naran Velji Arjan kama Mkurugenzi Mtendaji na Janet Akinyi Odhiambo kama Naibu Mwenyekiti wa Kitaifa.

Chama hicho kilisema mabadiliko hayo yanafuatia azimio la Halmashauri Kuu ya Taifa katika kikao kilichofanyika katika ofisi kuu ya chama mjini Karen.

“Tunarejea suala lililotajwa hapo juu kufuatia azimio la Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Roots katika kikao kilichofanyika Makao Makuu ya chama, tunathibitisha uteuzi wa viongozi wapya wa chama,” Sehemu ya taarifa ilisoma.

Wamae aliitwa Ijumaa na chama kufuatia matamshi yake.

Mkutano huo ulikuwa uwe wa hatua ya kinidhamu dhidi ya Wamae ambaye uhusiano wake na Wajackoyah umekua mbaya tangu uchaguzi mkuu wa Agosti 9.

"Kwamba kutokana na kuendelea kupotosha msimamo wa Chama, Chama kimekabiliwa na kejeli na sifa mbaya hadharani. Ni kwa ufahamu wetu kwamba mmeendelea kujitenga na chama na itikadi zake," barua ya wito ilisomeka.

Wamae alifika kwenye kituo hicho akiwa ameambatana na walinzi wake wenye silaha na wafuasi kadhaa.

Alidai kuruhusiwa kuingia ndani ya jumba hilo na wafuasi wasiopungua sita na kuandamana na waandishi wa habari ndani ya chumba hicho lakini mzozo ukatimbuka kwani wafuasi wake hawakuruhusiwa.

Akihutubia wanahabari, Wamae alisema hakufahamu ajenda ya mkutano huo wa nidhamu.

"Nimejitokeza kama raia anayetii sheria," alisema.

“Nimeitwa kufika mbele ya kamati ya nidhamu ya chama. Bado sijajua makosa yangu. nimejibu hivi punde.”

Wajackoyah alisema kuwa chama kilimwalika Wamae kueleza sababu kwa nini hapaswi kufukuzwa kwenye chama hicho, baada ya kudaiwa kuongea kwa zamu na uongozi wake wiki za hivi majuzi.