Maafisa wa kikosi cha kutoa ulinzi wa rais wamezuiwa kutumia miraa na muguka.
Katika notisi kutoka kwa mkuu wa kikosi hicho, marufuku hiyo inaanza kutekelezwa Julai tarehe 6. Notisi hiyo iliyotiwa saini na George Kirera imesema marufuku hiyo imetokana na athari za kiafya ambazo zimesababishwa na miraa na muguka kwa maafisa hao.
Notisi hiyo imesema maafisa wote wa ulinzi na raia wanaoishi ndani ya kambi ya kikosi cha ulinzi wa rais hawataruhusiwa kutumia zao hilo katika maeneo yao ya kazi. Notisi hiyo imesema afisa yeyote atakayekiuka agizo hilo atakabiliwa na hatua za kinidhamu.
Mwaka wa 2015, utafiti ulioonyesha kwamba matumizi ya miraa yanaweza kuathiri utendakazi wa mwanamme katika tendo la ngono na unaweza kusababisha mshutuko wa moyo .