Jamaa apuuza agizo la kukaa nyumbani na kuliwa na mamba Rwanda

Mwanaume mmoja nchini Rwanda ambaye alikiuka amri ya kukaa nyumbani ambayo inaendelea kutekelezwa nchini Rwanda na kuamua kwenda kuvua samaki ameuawa na mamba, Meya wa wilaya ya Kamonyi kusini mwa Rwanda amethibitisha .

Alice Kayitesi amesema kuwa tukio hilo lilitokea siku ya Jumatano asubuhi katika mto Nyabarongo.

"Alikua amekiuka sheria ya kukaa nyumban, alikua ni miongoni mwa watu wachache hapa ambao hawaonyeshi ushirikiano katika sheria hii ya kukaa nyumbani ili kuzuwia kusambaa kwa coronavirus ," Bi Kayitesi amesema.Serikali ya Rwanda iliweka amri ya kukaa nyumbani siku ya Jumapili kutokana na kuendelea kuongezeka kwa kasi kwa visa vya Covid-19.Rwanda imethibitisha kuwa na visa 40, vya maambukizi , idadi hiyo ikiwa ni ya juu zaidi kuriko mataifa mengine ya Afrika Mashariki.Kufungwa kwa shughuli za kiuchumi katika nchi hiyo kumwewaathiri watu wengi wenye kipato cha chini.Serikali imesema kuwa itawasaidia wale wanaohangaika wakati wa hatua kali za kudhibiti maambukizi.

Wakati huo huo idadi kubwa ya polisi wamesambazwa katika maeneo mbali mbali ya Rwanda ili kuhakikisha watu wanatekeleza amri ya kukaa nyumbani, kwa ajili ya kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona.Wale ambao wametajwa kuwa ni wafanyakazi muhimu, kama vile madaktari na wauguzi, wafanyakazi wa maduka ya jumla na waandishi wa habari, wanaruhusiwa kutoka nyumbani.

Kila baada ya kilomita 8 (maili tano ) mtu anaweza kupitia vituo vya ukaguzi vya polisi.Jumatatu, polisi walimpiga risasi na kumuua mwanaume mmoja viungani mwa mji wa Kigali ambaye walisema alikiuka amri ya kukaa nyumbani.Polisi walisema kuwa alikua anajaribu kupigana na maafisa.Kumekua na ripoti za wafanyakazi wa kazi za jua kali ambao kwa sasa hawana kipato wanaojaribu kutoroka kutoka mji mkuu Kigali kujiunga na familia zao zilizoko vijijini, wanaotembea mwendo mrefu kutokana na kupigwa marufuku kwa usafiri wa umma.