Kipchoge akiri kuwa mtulivu kabla ya jaribio lake la Ineos1:59 challenge

Bingwa wa dunia katika mbio za Marathon kwa wanaume Eliud Kipchoge anasema yuko mtulivu kabla ya jaribio lake la kesho la kukimbia Marathon, kwa chini ya masaa mawili huko Vienna.

Mbio hizo maalum zitaandaliwa kesho asubuhi na Kipchoge atasindikizwa na zaidi ya waweka kasi 20. Kipchoge ambaye amekuwa akijitayarisha kwa zaidi ya miezi minne chini ya kocha wake Patrick Sang anasema ana imani ataweza kufaulu.

Hayo yakijiri, Russia Sevens Academy itakua timu ya kwanza kuwasili kwa michuano ya Safari Sevens ya mwaka huu itakayoandaliwa Oktoba tarehe 19-20 uwanjani RFUEA.

Timu hiyo inafunzwa na gwiji wa Sevens Waisale Serevi na watawasili Nairobi leo kwa kambi ya wiki moja kabla ya kipute hicho.

Afisa mkuu wa KPL Jack Oguda anajikakamua huku kukiwa na fununu kua huenda ligi hiyo ikasimamishwa kutokana na ukosefu wa fedha.

Oguda anasema taarifa hizo si za kweli na ligi hiyo itaendelea. Ligi hiyo imekua ikiyumbayumba kifedha tangu Sportpesa kusitisha ufadhili wake baada ya leseni yao kufutiliwa mbali.

Baadhi ya vilabu havijawalipa wachezaji wake huku marefa pia wakiwa hawajalipwa.