Maajabu! Jamaa ajitia kitanzi baada ya kujichimbia kaburi, Homa Bay

Mwanamume mwenye umri wa miaka 50 aliyekuwa amechimba kaburi Lake mwenyewe miezi michache iliyopita anadaiwa kujitia kitanzi katika eneo la Kasipul Kabondo, Kaunti ya Homa Bay.

Mwili wa Charles Moseti ulipatikana ukining’inia kwa kamba iliyokuwa imefungwa kwa paa ndani ya nyumba alimokuwa akilinda katika kijiji cha Got Okombo mwishoni mwa wiki. Kufikia kifo chake Moseti alikuwa akifanya kazi ya ulinzi katika nyumba moja.

Kiini cha hatua yake bado hakijabainika. Wakaazi walisema hakuwa hata amezozana na mtu yeyote.

Kamanda wa polisi kaunti ndogo ya Rachuonyo Charles Barasa alisema kwamba walikuwa wamepata ripoti kuwa Moseti alikuwa amejichimbia kaburi katika boma lake atakamo zikwa akifariki.

“pasta wake alituarifu kwamba alikuwa amechimba kaburi kwake miezi kadhaa iliyopita. Hii ilikuwa kuandaa familia yake kwa kifo chake,” Barasa alisema.

Hata hivyo, Barasa alisema hapakuwepo jambo linalohusisha kifo chake na tukio lolote kutoka nje.

Kamanda huyo wa polisi anasema Moseti hakuacha barua yoyote kueleza kilichokuwa kimechangia kujiua kwake. “ Kifo chake huenda kilichochewa na sababu zake za kibinafsi lakini bado tunafanya uchunguzi kupata maelezo zaidi kuhusu kifo hicho,” alisema.

Mwili wake ulipelekwa katika hifadhi ya maiti ya hospitali ya Rachuonyo mjini Oyugis.